SOMO:KATIKA YESU KILA JARIBU LINA MLANGO WA KUTOKA
ZABURI 139:11-16;
MATHAYO 4:1-11
*SOMO LA MAHUBIRI: DANIELI 3:19-23*
WIMBO: TMW 86
*UTANGULIZI*
Nebukadreza mfalme wa Babeli aliishinda Yerusalemu na kuwachukua watu mateka wakiwepo kutoka katika nyumba ya kifalme, huu ulikuwa wakati wa Mfalme Yehoyakimu wa Yuda, pia vyombo vya nyumba ya Bwana vilichukuliwa hadi Babeli. Hii ilikuwa hukumu ya Mungu kwa uasi wa ufalme wa Yuda. Kwa upande mwingine huu ulikuwa mwanzo wa mpango wa Mungu ndani ya uhamisho (Danieli 1:1-2). Mateso na majaribu hayamaanishi kwamba Mungu hayupo. Mfalme Nebukadreza akamwagiza Ashpenazi Mkuu wa matoashi amtafutie vijana wa Kiebrania wenye vinasaba vya kifalme, wasio na mawaa, wazuri wa uso, wajuzi wa hekima, werevu kwa sababu ya maarifa yao, wenye kufahamu elimu, watakaoweza kusimama katika jumba la kifalme. Ili wafundishwe lugha ya Wakaldayo, elimu ya kifalme, na utamaduni mpya. Vijana hawa wanne hata majina yao yalibadilishwa kama jaribio la kubadili utambulisho wao wa kiimani lakini ilishindikana walibaki na Imani yao (Danieli 1:3-7). Vijana hao ni: Danieli – Belteshaza Hanani – Shadraka Mishaeli – Meshaki Azaria – Abednego Hawa vijana walionesha msimamo usiokuwa wa kawaida walikataa kula chakula cha kifalme walichoagizwa walishwe miaka mitatu wao wakala mtama na maji na afya zao zikawa nzuri kuliko wale vijana waliokula chakula cha mfalme. Mungu aliwapa neema na hekima na mwisho wa siku walipoingizwa mbele ya mfalme kwa usaili walionekana kuwa bora mara kumi zaidi ya waganga na wachawi waliokuwa katika ufalme wake (Danieli 1:-20). Ilitokea kwamba mfalme aliota ndoto ambayo ilifadhaisha roho yake na usingizi kumwacha. Alitoa amri ya kuitwa kwa waganga, wachawi, wasihiri na wakaldayo ili watoe tafsiri ya ndoto ambayo alikuwa ameisahau. Wakaldayo wakajibu na kusema kuwa Hapana mtu duniani awezaye kulionesha neno hili la mfalme kwa maana Hapana mfalme wala bwana aliyetaka neno kama hili. Ni neno la ajabu analotaka mfalme, hakuna awezaye kumwonesha mfalme neno hilo ila miungu wasio na kikao Pamoja na mwenye mwili. Mfalme akakasirika mno akatoa amri ya kuua wenye hekima wote wa Babeli (Danieli 2:1-12). Wenye hekima wakawa wanatafuta kuuawa na Danieli na wenzake ambao hawakuwepo wakati wale wengine wanashindwa akawa anawatafuta Pamoja na wenzake ili wauawe. Danieli akamuuliza Arioko Akida wa walinzi wa mfalme aliyetumwa kuwaua, akasema, mbona amri ya mfalme inau kali hivi? Akaomba aingie kwa mfalme na akaomba apewe muda wa Kwenda kutafuta hiyo tafsiri. Danieli akawapasha Habari wenzake watatu kwamba waombe rehema na kupewa tafsiri au siri ya ile ndoto. Usiku Danieli akapewa ile ndoto ambayo mfalme aliota Pamoja na tafsiri yake. Mfalme Aliona sanamu kubwa. Kichwa cha dhahabu – Babeli (Ufalme wa Nebukadreza). Kifua na mikono yake ya fedha – Ufalme unaofuata. Tumbo na viuno vyake vya shaba – ufalme mwingine Miguu ya chuma nyayo zake nusu chuma na nusu udongo – Falme zinazogawanyika. Maana yake falme hizi ni za muda na dhaifu. Jiwe lililochongwa bila mikono, liliipiga sanamu miguu ikavunja vipande vipande huu ni ufalme wa Mungu wenye nguvu na utadumu milele (Danieli 2:13-45). Mfalme Nebukadreza akamtukuza Mungu akampa Danieli cheo cha kuwa mkuu juu ya Uliwali wote na mkuu wa wote wenye hekima wa Babeli na Danieli akawaombea nafasi wale wenzake watatu (Danieli 2:46-49). Tunapoanza na masilimulizi ya sura ya tatu inaonekana kuwa mfalme Nebukadreza aliazimia kupinga maelekezo ya Mungu ambayo yalitolewa na Danieli katika tafsiri ya ndoto. Aliamua kutengeneza sanamu ya dhahabu tupu kama kuashiria kuwa ufalme wake hautakoma kinyume na ujumbe wa ndoto. Nebukadreza aliamuru watu wote waabudu sanamu ile na kutofanya hivyo ilitafsiriwa kama kosa la uhaini (treason). Watu wote walitii isipokuwa watatu (Shadraka, Meshaki na Abednego). Kufuatia habari zilizopo sura ya pili, Danieli alipandishwa cheo na hivyo akawa anatumika ikulu, kwa hiyo hakujumuika nao. Huu ulikuwa mtihani wao na Danieli alipewa mtihani wake peke yake baadaye (Danieli 6). Inaonekana watu walikuwa wanawafuatilia wakagundua kuwa hawa jamaa wamegoma kuabudu sanamu, wakapeleka taarifa kwa mfalme Nebukadreza. Inaonekana kulikuwa na wivu wa kisiasa kwani hawa wageni walipewa nafasi za utawala. Nebukadreza hakutaka kuwachukulia hatua kwa maneno ya kusikia akawaita na kuwahoji. Je, ni kweli mmekataa kuabudu sanamu? Akawapa nafasi ya kufanya hivyo na kwamba wakikataa watatupwa kwenye tanuru la moto ili aone ni mungu yupi atakaye waokoa na mkono wake na pia na tanuru la moto. Na hapa ndipo alipokosea kumhusisha Mungu katika hoja zake. Wakamjibu kuwa hawakuwa na haja ya kujitetea, kosa wanalijua lakini Mungu wanayemtumikia atawaokoa na tanuru na mkono wa mfalme. Wakasema wazi kuwa hawakuwa tayari kutumikia miungu ya Nebukadreza wala kuabudu sanamu yake (Danieli 3:1-18). Ndipo linafuata somo letu la mahubiri (Danieli 3:19 -23). Mfalme Nebukadreza akastaajabu, akainuka haraka, akauliza kuwa je, hatukutupa watu watatu wakiwa wamefungwa? Mbona anaona watu wanne wamefunguliwa, wanatembea Katikati ya moto na hauna madhara na yule wa nne ni mfano wa mwana wa miungu. Akawaita Shadraka, Meshaki na Abednego kuwa ni watumishi wa Mungu aliye juu kuwa watoke nje. Nebukadreza akamhimidi Bwana na kuweka amri kwa kila kabila za watu, kila taifa na kila lugha kuwa yeyote atakaye nena neno lolote lisilopasa juu ya huyo Mungu wa Shadraka, Meshaki na Abednego atakatwa vipande vipande na nyumba zao kufanywa jaa kwa kuwa hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii. Kisha akawapandisha vyeo katika wilaya ya Babeli (Danieli 3:24-30). 2. *DANIELI 3:19-23 HASIRA YA MFALME NA MOTO MKALI DHIDI YA SHADRAKA, MESHAKI NA ABEDNEGO* Shadraka, Meshaki na Abednego walikataa kuabudu sanamu ya Mfalme Nebukadreza kwa sababu ya uaminifu wao kwa Mungu mmoja, aliye hai na ndiye pekee anapaswa kuabudiwa. Mfalme akawatisha juu ya uamuzi wao na kwamba angewachoma moto. Bado walikaza uamuzi wao na kutamka wazi kwamba moto hauna nguvu juu ya nguvu za Mungu. Mfalme kwa hasira akaamuru tanuru lichochewe mara saba kuliko kawaida. Hasira ya Nebukadreza inadhihirisha uasi wa mwanadamu dhidi ya Mungu. Hasira ya mfalme ilitokana na ushuhuda wa kishujaa uliotolewa na wale vijana watatu. Kabla hawajatoa msimamo wao mkali juu ya Imani yao katika Mungu aliye hai alikuwa akiwasemesha kama watoto wake. Hawakuona aibu kumshuhudia Mungu wao. Mfalme akatumia tanuru ambayo inasimama kama ishara ya hukumu, mateso, mauti. Kwa hakika tunaweza kuona kivuli cha msalaba katika tukio hili. Kwani hata Yesu alihukumiwa na mamlaka za dunia hii kama akina Shadraka, Meshaki na Abednego walivyohukumiwa. Baada ya moto huo mkali kuandaliwa walitafutwa vijana wenye nguvu, wakawafunga watumishi wa Mungu na kuwatupa katika tanuru la moto, wale waliowabeba Shadraka, Meshaki na Abednego moto uliwalamba wenyewe wakafa. Mle ndani wakaonekana akina Shadraka, Meshaki na Abednego wakiwa huru hawajafungwa tena. Mfalme alishangaa mno kwani halikuwa tukio la kawaida. Katika tafsiri ya toleo la Septuagint inasema, mfalme alishituka kusikia wale vijana wanne wakiimba nyimbo za sifa ndani ya tanuru. Moto ulikula Kamba zilizowafunga lakini haukugusa nguo zao wala nywele wala hata harufu tu ya moto hawakuwa nayo. Mle ndani akina Shadraka, Meshaki na Abednego hawakuwa peke yao walikuwa na mtu wa nne aliyeonekana kuwa ni mwana wa Mungu. Kumbe Yesu aliingia nao katika tanuru. Sio lazima Mungu akaepushe na majaribu au mateso wakati mwingine anakwenda na wewe, usiogope hupo peke yako. Hatuna uhakika kama akina Shadraka, Meshaki na Abednego walijua kuwa wapo Pamoja na Yesu mle ndani ya tanuru ya moto. Kwa hiyo tuwe tunaona au hatuoni Yesu yupo Pamoja nasi. Mfuasi wa Kristo pia ana tanuru za aina mbali mbali ambazo anakutana nazo katika maisha. Kuna tanuru ambazo mtu mwenyewe anajitengenezea, zipo ambazo zinatengenezwa na Shetani na nyingi zinaandaliwa na Mungu. Kwa hiyo Mungu anaweza kutuokoa kutoka katika majaribu au akatuwezesha kubeba au kushinda jaribu hilo.
3.*KATIKA YESU KILA JARIBU LINA MLANGO WA KUTOKA*
Habari za vijana wanne Danieli, Shadraka,Meshaki na Abednego zinatuonesha kuwa vijana hawa walikuwa Hodari na wenye ufanisi mkubwa tangu kuitwa kwao. Ufanisi wao haukuwa kwa sababu ya elimu tu wala nafasi zao nzuri serikalini bali ulitokana na msingi wa kiroho ambao uliongoza maisha yao yote. Ushindi wao juu ya majaribu haukupatikana katika siku moja bali ulishuhudia aina ya watu walivyo na jinsi walivyoishi na Mungu. (a) Walikuwa wameandaliwa toka nyumbani na mfalme alitafuta watu wenye sifa. (b) Walikuwa na uamuzi moyoni juu ya kumtii Mungu. Danieli na wenzake waliazimia moyoni kutojitia unajisi na vyakula vya mfalme hata kama vilionekana kuwa vyenye sifa wao wakala mtama na kunywa maji (Danieli 1:8). Kwa hiyo mafanikio yao yalianza moyoni kwa uhusiano sahihi na wauaminifu na Mungu. (c) Walidumisha maisha ya utakatifu na hofu ya Mungu Katikati ya maisha ya kipagani. Shadraka, Meshaki na Abednego waliposhurutishwa kusujudia sanamu walikataa hata walipotishwa na tanuru la moto. Walichagua kuwa waaminifu kwa Mungu na kuuacha usalama wa maisha yao mikononi mwa Mungu (Danieli 3). (d) Walikuwa watu wa maombi na kumtegemea Mungu kila siku. Maisha ya ushindi hayaanzi na mbinu bali na uhusiano. Danieli alipata ushindi kwa sababu aliishi mbele za Mungu kila siku (Danieli 6:10). Danieli hakuanza kuomba baada ya tishio bali aliomba kama ilivyokuwa desturi yake na akaendelea hata baada ya amri ya kutokuomba kutangazwa. Hatuanzi kuomba baada ya kuingia majaribuni tunahitaji kuishi maisha ya maombi. (e) Mungu alisimama upande wao. Moto haukuwaunguza (Danieli 3) na simba hawakumwangamiza Danieli (Danieli 6). Mungu hatuzuii tusipitie majaribu bali anapita nasi katika majaribu. Alienda na akina Shadraka ndani ya tanuru la moto, alienda na Danieli ndani ya tundu la simba na kuwafumba vinywa vyao. Mungu hakungoji nje bali anaenda Pamoja nawe. Majaribu ni njia ya kuuendea ushindi. Ndio maana wapo ambao hufika kwenye ushindi na wengine hurudia njiani. (f) Walitumia ujuzi na karama zao kwa utukufu wa Mungu. Hawa vijana wanne walikuwa na hekima, maarifa na nafasi za juu katika serikali kule Babeli lakini walielekeza utukufu kwa Mungu sio kwao. Katika somo letu tunajifunza kuwa Kristo yupo na watu wake katika moto. Yesu hatuokoi akiwa mbali kama mtazamaji bali anaingia katika mateso, anaingia mwenyewe katika tanuru la moto uliokolezwa mara saba. Majira haya tumeanza safari ya Kwaresma tangu jumatano ya majivu (18/02/2026), ni majira ya kutafakari mateso ya Bwana Yesu, kutubu dhambi na kujifunza juu ya tumaini la msalaba. Neno letu limetupeleka Babeli kwenye tanuru la moto ambako vijana wale watatu walikataa kusujudia sanamu, wala miungu ya Wakaldayo. Walikuwa tayari kupitia mateso hata kifo kwa ajili ya Imani yao. Kipindi hiki cha kwaresma tunamwona yule Yesu ambaye alikuwa na wale vijana ndani ya tanuru la moto, anauendea msalaba kwa ajili ya ukombozi wetu wanadamu. Kuonekana kwake ndani ya tanuru ulikuwa udhihirisho wa Yesu kabla hajazaliwa katika mwili. Uwepo wa Yesu ndani ya tanuru la moto ni ujumbe kwamba Mungu hayuko mbali na mateso ya watu wake. Haangalii toka toka mbinguni bali alifanyika mwili na kupita nasi katika mateso. Mungu anaingia ndani ya moto wa dhambi ambazo zilitutesa, hii ndio injili ya Kwaresma, ukombozi kwa njia ya msalaba. Pamoja na Yesu ndani ya tanuru akina Shadraka walikuwa huru wakitembea, hawajafungwa na wala hawakuungua. Moto upo lakini hauwezi kutuangamiza, kifo kipo lakini Yesu ni mshindi w amauti, mateso yapo lakini sio mwisho kwa sababu Yesu yumo ndani ya moto Pamoja nasi. Ujumbe wa msalaba unasema, Yesu huokoa si kwa kuondoa mateso kwanza, bali kwa kuwa Pamoja nasi ndani yake. Tukiangalia masomo yetu yote matatu tuliyopewa katika kalenda Zaburi 139:11-16; Mathayo 4:1-11 na Danieli 3:19-23 yote yanatutaka tuelekeze macho yetu kwenye siri ya ushindi wa Mungu Katikati ya giza, majaribu na moto. *Zaburi 139:11-16* Mungu alimwona Daudi na kumuandaa kabla ya vita. Hakuna giza linaloweza kumficha mtu mbele za Mungu. Mungu alimuumba mtu kwa jinsi ya ajabu tangu tumboni na kupanga siku zake zote. Kabla ya jaribu halijaja Mungu tayari anajua na ameandaa ushindi. Tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu kiasi kwamba maarifa hayo hatuwezi kuyafikia na kuyaelewa. Kwa hiyo kwa kufuata Zaburi yetu hatuingii vitani, majaribuni peke yetu bali tunaingia tukiwa tunajulikana na Mungu. Mungu hutuandalia mlango wa kutoka kabla hatujaingia. Yeye hutangaza mwisho tangu mwanzo (Isaya 46:10). *Mathayo 4:1-11.* Yesu anajaribiwa jangwani, tena alipelekwa na Roho Mtakatifu. Alipata majaribu matatu: Jaribu la mwili, mkate; jaribu la kujionesha aruke kutoka hekaluni na jaribu la mamlaka na umiliki bila msalaba. Yesu alichukua mamlaka kwa njia ya msalaba na kumiliki vyote (Waefeso 1:18-23). Katika majaribu hayo yote Yesu alishinda kwa Neno la Mungu kila mara akisema, Imeandikwa … Kama Yesu alishinda kwa neno, na sisi hatuwezi kushinda kwa nguvu zetu bali kwa Neno ambalo pia ni Yesu mwenyewe. Katika somo la Danieli *(Danieli 3:19-23)* tumeona wale vijana wakiwa na mtu wa nne ndani ya moto. Mungu haji kabla ya jaribu, huingia ndani ya jaribu Pamoja nasi. Kumbe moto ambao ulipanga kutuangamiza unageuka kuwa mahali pa ufunuo wa uwepo wa Mungu na mahali pa Mungu kutukuzwa na kuabudiwa na watu wote.
Uwe na Kwaresma nje
Monthly Archives: February 2026
MAHUBIRI YA IBADA YA JUMATANO YA MAJIVU TAREHE 18/02/2026
Wazo:RARUENI MIOYO YENU
Yoeli 2:15-20*
*UTANGULIZI*
Wapendwa katika Kristo Yesu, neema na amani zitokazo kwa Mungu Baba na Bwana wetu Yesu Kristo ziwe nanyi nyote. Amina.
Leo tunaingia katika kipindi cha Kwaresma, tukianzia Jumatano ya Majivu. Ni kipindi cha kutafakari mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo, kujichunguza, kutubu, na kurejea kwa Mungu kwa moyo wote.
Neno la Bwana kupitia nabii Yoeli linatuita kwa sauti kuu:
“RARUENI MIOYO YENU.”
Siyo kurarua mavazi, siyo ishara za nje tu, bali ni mabadiliko ya ndani kabisa.
2. *Ufafanuzi (Yoeli 2:15–20)*
Nabii Yoeli aliishi wakati ambapo taifa la Israeli lilipitia janga kubwa – uvamizi wa nzige uliharibu mazao, uchumi ukaporomoka, njaa ikaenea. Hali hii haikuwa tu tukio la kawaida la asili, bali ilikuwa ishara ya kiroho – watu walikuwa wamemwacha Mungu.
Ndipo Mungu akatoa wito:
“Pigeni tarumbeta Sayuni” – Tangazeni mkutano mtakatifu.
“Kusanyeni watu, watakaseni mkutano.”
Hata wazee, watoto, wachanga, na hata wanandoa waliokuwa kwenye chumba cha harusi waliitwa kuja mbele za Mungu.
Kwa nini?
Kwa sababu tatizo lilikuwa la kitaifa na suluhisho lilikuwa toba ya pamoja.
3. *UFAFANUZI WA MADA: “RARUENI MIOYO YENU”*
Katika utamaduni wa Kiyahudi, mtu alipokuwa na huzuni au toba, alirarua mavazi yake kama ishara ya majonzi. Lakini Mungu anasema:
“Rarueni mioyo yenu wala si mavazi yenu.” (Yoeli 2:13)
Hapa Mungu anasisitiza mambo matatu:
(i) Toba ya kweli ni ya ndani
Siyo machozi ya nje tu.
Siyo kufunga bila kubadilika.
Siyo kwenda kanisani bila kuacha dhambi.
Ni moyo uliovunjika mbele za Mungu.
(ii) Mungu anatazama moyo
Tunaweza kuwaficha watu, lakini hatuwezi kumficha Mungu.
Anaona kiburi, chuki, wivu, uasherati wa siri, dhambi za moyoni.
(iii) Mungu ni mwenye rehema
Yoeli anasema:
“Kwa maana yeye ni mwenye neema, rehema, si mwepesi wa hasira.”
Hii ndiyo tumaini letu katika Kwaresma – Mungu hatuiti ili atuangamize, bali ili atuokoe
*A. SHERIA – TUNAHITAJI KURARUA MIOYO YETU*
Je, mioyo yetu ikoje?
Je, tunaishi maisha ya mazoea tu ya kikristo?
Je, ibada imekuwa desturi tu?
Je, tunashika nafasi kanisani lakini mioyo iko mbali na Mungu?
Kwaresma ni wakati wa kujitazama:
Mahusiano yetu na Mungu yakoje?
Maisha ya maombi yakoje?
Tumeacha dhambi kweli au tunazificha?
Mungu anatuita: Rarua moyo wako.
*B. INJILI – MUNGU ANARUDISHA NA KUJESHA*
Yoeli 2:18–19 inaonyesha Mungu akihurumia watu wake.
Baada ya toba ya kweli:
Mungu aliahidi kurejesha mavuno.
Aliahidi kuondoa aibu.
Aliahidi kuwalinda dhidi ya adui.
Hii ni picha ya Kristo.
Katika Kwaresma tunamwangalia Yesu:
Anaenda Yerusalemu kwa ajili yetu.
Anakubali mateso kwa ajili ya dhambi zetu.
Anamwaga damu ili kutusafisha.
Tunaporarua mioyo yetu kwa toba, Kristo anatujaza rehema na msamaha.
Hakuna dhambi kubwa kuliko neema ya Mungu
*MWITO WA MAISHA MAPYA*
Yoeli anawaita watu wote – wazee, vijana, watoto.
Maana yake:
Hakuna aliye nje ya wito wa toba.
Hakuna aliye mkamilifu asiyohitaji neema.
Katika Kwaresma hii:
Rudisha ibada ya familia.
Ongeza muda wa maombi.
Samehe waliokukosea.
Acha dhambi inayokutesa.
Jitoe zaidi katika huduma.
Hiyo ndiyo “kurarua moyo.”
*MAANA YA JUMATANO YA MAJIVU*
Majivu ni ishara ya:
Unyenyekevu
Kukumbuka kwamba sisi ni mavumbi
Kutubu na kurejea kwa Mungu
Lakini kumbuka:
Majivu kwenye paji la uso hayasaidii kama moyo haujabadilika.
Mungu hataki alama ya nje tu.
Anataka moyo uliotubu.
*HITIMISHO*
Wapendwa,
Yoeli anatufundisha kuwa:
Toba ya kweli huanzia moyoni.
Mungu ni mwingi wa rehema.
Baada ya toba, kuna urejesho.
Leo, Mungu anakuita binafsi:
“Rarua moyo wako.”
Usingoje kesho.
Usingoje Pasaka.
Anza leo.
Kristo yuko tayari kukusamehe, kukuponya, na kukurejesha.
*SALA YA KUFUNGA*
Ee Mungu wetu mwenye rehema,
tuvunje mioyo yetu ya mawe, utupe mioyo mipya.
Tujalie toba ya kweli katika kipindi hiki cha Kwaresma.
Utusafishe kwa damu ya Yesu Kristo,
ili tuishi maisha mapya ya utakatifu na upendo.
Katika jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu.
Amina.
Ev.John
whatsapp:0768386606
KKKT DKU SIKU YA BWANA YA 7 KABLA YA PASAKA
*IBADA YA TAREHE 15 FEBRUARI 2026*
SIKU YA BWANA YA 7 KABLA YA PASAKA (QUINQUAGESIMA/ESTOMIHI)
*YESU AIENDEA NJIA YA MATESO YERUSALEMU*
ZABURI 48:1-8; RUMI 11:25-27
*SOMO LA MAHUBIRI: MATHAYO 17:22-23*
WIMBO: TMW 415
MAFAFANUZI
1. *UTANGULIZI*
Katika Injili ya Mathayo Yesu anatabiri juu ya mateso, kifo na kufufuka kwake mara tatu. Hii inaonesha kuwa mateso na kifo cha Yesu hayakutokea kwa bahati mbaya bali yalikuwa sehemu kamili ya mpango wa Mungu wa wokovu. Utabiri huu unajitokeza katika Mathayo 16:21–23; 17:22–23; 20:17–19.
Utakachokiona katika utabiri huo ni kwamba, hata kama alizungumza habari za kutiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani, kuteswa na kuuawa, bado kila mara alimaliza na kufufuka kwake. Maneno mengine yaliweza kukosekana, kwa baadhi ya tabiri; lakini kila mara kufufuka kumejitokeza. Hii ina maana kwamba, hata kama mateso ilikuwa lazima, Yesu alikuwa anatazama mbele kwenye matokeo ya hayo yote. Hapuuzii uwepo wa mateso dhihaka na kifo, lakini anaona kwamba hayo yanatumika kumfikisha kwenye utukufu. Na katika kuyasema, hafichi. Anaweka wazi kuwa yatampata, Yeye mwenyewe, si mwingine. Mkazo huo ulikuwa wa muhimu ili kutimiza unabii wa Isaya 53 kuteswa kwa masihi (the Suffering Messiah). Na hii ina maana kubwa katika theologia. Kuwa mfuasi wa Yesu hakumwepushi mtu na mateso au changamoto, bali kuna mthibiitsha kuwa yeye ni nani hata anapkuwa katika mateso. Na uthibitisho hapo ni kwamba, mateso yajapokuwa makali kiasi gani, ushindi upo.
Wanafunzi walipaswa kujifunza maana ya ufuasi lakini hilo lilifichwa machoni pao, aliwaambia mtu akitaka kunifuata ajikane nafsi yake auchukue msalaba wake (Mathayo 16:24).
*Mathayo sura ya 17 in sehemu kuu tatu:*
(a) *Mathayo 17:1-13 Utukufu wa Yesu unaofunuliwa*
Mistari nane ya kwanza inahusu Yesu kugeuka sura (17:1-8). Yesu alionekana katika utukufu wa hali ya juu sana na sauti ya Baba ikathibitisha utambulisho huo. Hiki kilikuwa kilele cha ufunuo wa Yesu. Halafu yanafuata mafundisho kuhusu Eliya/Yohana Mbatizaji (17:9-13). Yesu ni Mwana wa Mungu na utimilifu wa torati na manabii. Lakini hali halisi ni mateso. Yohana mbatizaji alikuja wakamtesa. Vivyo hivyo watamtenda Mwana wa Adamu.
(b) *Mathayo 17:14-21 Udhaifu wa Wanafunzi na dai la Imani*
Waliposhuka bondeni wanafunzi waliendelea kushuhudia hali halisi ya dunia, kijana aliteswa na pepo na wanafunzi waliteswa na Imani ndogo. Kwa hiyo wale wanafunzi watatu waliorudi na Yesu toka mlimani walikutana na maumivu ya dunia ambayo walitamani kuyakimbia waliposema wajenge vibanda 3.
Wanafunzi 9 waliobaki bondeni wakati Yesu ameenda mlimani na wanafunzi 3 walishindwa kutoa pepo. Ndipo Yesu akatoa fursa hiyo kufundisha kuwa Imani ni kama chembe ya haradali. Nguvu ya huduma haitoki kwa mwanadamu bali inatoka kwa Mungu kupitia Imani.
(c) *Mathayo* *17:22* – *27* Njia ya Msalaba na Maisha ya wanafunzi duniani
Sehemu hii inahusu utabiri wa Yesu juu ya kuteswa, kufa na kufufuka kwake. Halafu ilifuata habari ya kodi na uhuru wa mwana. Kwa hiyo utukufu wa Yesu unaelezwa kwa njia ya msalaba. Na msalaba ni alama ya unyenyekevu na mateso. Kazi ya yake ni kumfanya mtu anyenyekee kwenye kila mfumo. Kwa watawala – mtu awe mnyenyekevu; katika kuutumia uhuru wake, asijiinue, napo pia awe mnyenyekevu. Kazi ya mateso na msalaba ni kumleta mtu kwenye ukuu wa kweli – yaani ukuu wenye unyenyekevu na uliojaa upendo.
Mathayo 17:22-23 tunakutana na siri ya mpango wa Mungu juu ya wokovu na hiki ndicho kitovu cha sura ya 17. Baada ya kuona utukufu pale mlimani, mateso ya dunia, udhaifu wa imani ya wanafunzi, Yesu anafunua sababu ya yote hayo na suluhisho lake. Hii ni njia ya msalaba na ufufuo. Kung’aa kusingeeleweka na mateso ya dunia yangetupeleka kukata tamaa na kukosa matumaini .
Mathayo 17:24-27 ni aina ya maisha ya wanafunzi baada ya kujua siri hiyo kuu. Wanaishi kwa unyenyekevu, wanalipa kodi ili kutowakwaza wengine, wanatumia uhuru wao kwa kwa unyenyekevu unaotokeza upendo na uwajibikaji.
2. *MATHAYO* *17:22* – *23* *UTABIRI* *WA* *PILI*
Walipokusanyika (walipokaa) Galilaya Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua na siku ya tatu atafufuka. Wakasikitika sana. Hili si tangazo la kawaida, wala si tangazo la hofu na kushindwa bali ni taarifa ya mpango wa kazi ulioko mbele yao. Wao walikuwa hawaoni, kwa hiyo anawaambia mapema: msishituke, mpango unaofuata ni huu. Taarifa hii ilikuwa inawaandaa kisaikolojia. Na Kitheologia tunasema, ikiwa mtu anazunguka huko na huko akisema habari ya kifo chake na kufufuka kwake hata kabla havijatokea, ama ni kichaa au ni Mwana wa Mungu. Na kwa habari ya Yesu, alikuwa anawaambia jambo ambalo walikuwa hawajui. Hata kama mimi nipo katika mwili, ”Mwana wa Adamu”, mimi nina asili ya uungu. Hasemi kwa maneno, lakini maana ya kazi na ratiba anayoonesha inaibua hayo.
*Mwana wa Adamu*
Kwa mara ya kwanza habari ya Mwana wa Adamu inaonekana katika Danieli 7:13-14. Danieli anaona maono ya mbinguni, ambako kuna viumbe wa rohoni. Hata hivyo, kuna jambo la peke, anamwona mtu mwenye mwonekanekano au mfano wa mwanadamu – ndio maana ya Mwana wa Adamu. Danieli haelezi kirefu. Lakini alichokiona kimekuja kuwa wazi katika Yesu Kristo. Mungu ameuchukua mwili na kwa huo anatumia kuwakomboa wanadamu. Kwa huo atakuwa miongoni mwa watu – Mungu pamoja nasi; kwa huo atateswa. Alishuka na kunyenyekea lakini kunyenyekea kwake kumekuwa sababu ya wokovu kwa ulimwengu. Maana kama angebaki katika roho, hakuna mtu angethubutu kuunyosha mkono wake na kumtesa. Na hii ndio siri ya Kimasihi, na hapa neno Mwana wa Adamu limekuwa jina linaloficha siri kuu. Kuielewa unahitaji utulivu. Anajiita Mwana wa Adamu makusudi – anaficha asili yake halisi.
*Mwana wa Adamu anakwenda,* hili linaonesha kuwa ni safari ya makusudi kuuendea msalaba. Mungu katika mwili (Mwana wa Adamu) anakwenda msalabani. Kwa asili mwanadamu hukimbia hatari lakini Yesu anakaza uso kuyaendea mateso. Anayaendea mateso kwa upendo mkubwa wa kujitoa kwa sababu anajua nini anachofanya. Amekuja Kutenda mapenzi ya Baba, anajitoa kwa ajili ya rafiki zake ambao wana dhambi sio watakatifu. Yohana 15:13 Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Asingeweza kuyafanya hayo kama asingekuwa Mungu. Na sisi hatuwezi kujitoa kwa ajili ya wengine, Mungu asipokuwa ndani yetu. Hatuwezi kama ndani yetu hakuna Kristo.
*Anakwenda kutiwa au kukabidhiwa* (Kiyunani – paradidosthai). Anakaribia kukabidhiwa mikononi mwa wanadamu. Si tu kwamba atasilitiwa bali anakabidhiwa kwa makusudi yaliyomo katika mpango wa Mungu. Ni mpango wa Mungu unaotendeka kupitia mikono ya waovu. Yesu hasukumwi na mwanadamu bali anakabidhiwa kulingana na mpango wa Mungu wa wokovu (Isaya 53; Mdo 2:23). Ndio maana hili halikuweza kutendeka hadi wakati wa Mungu ulipotimia.
*Watamwua:* Hii inasisitiza kuwa tukio hilo ni la uhakika sio uwezekano. Hata kama Petro alijitahidi kusema, Hasha, hilo halikupati wewe alikuwa anapingana na mpango wa Mungu ambao ulikuwa lazima kwa vile hapakuwa na njia nyingine ya kuleta wokovu isipokuwa kupitia kifo cha Yesu, ndio maana alimwambia nenda nyuma yangu Shetani.
*Siku ya tatu atafufuka:* Mungu Baba ndiye aliyemfufua. Kufa na kufufuka kwa Yesu ndio msingi wa Imani yetu. Hata Kiri zetu za Imani ya Mitume na Nikea zinasimama katika Imani hiyo ya kwamba aliteswa, akafa na siku ya tatu alifufuka kutoka kwa wafu. Hata mahubiri ya Petro (Mdo 2; 3; 4) yalijengwa katika Habari za kufa na kufufuka kwa Yesu. Mtume Paulo katika 1 Korintho 15:3-4 kwamba alikufa na kufufa kama yaneyavyo maandiko (15:14) anaonesha kuwa bila kufa na kufufuka kwa Yesu, Imani yetu ni bure. Je, kanisa la leo mkazo wa mafundisho yake upo wapi? Ikiwa tutaacha kusisitiza haya, ni wazi kwamba tunajenga kwenye msingi usio sahihi.
*Wanafunzi wakasikitika sana au kupita kiasi:* Hawakuelewa ufufuo hadi Yesu alipokufa na kufufuka ndipo macho yao yalifumbuliwa. Walikuwa na uhusiano wa karibu na Yesu na wasijue hatima yake.
3. *YESU AIENDEA NJIA YA MATESO YERUSALEMU.*
Hii ni jumapili ya mwisho kabla ya majira ya Kwaresma (Quinquagesima). Kanisa linaanza kuelekeza macho toka utukufu Kwenda msalabani. Kutoka miujiza Kwenda mateso yaletayo ukombozi wa kudumu, wokovu kamili katika kifo na ufufuo wa Yesu. Jumapili hii ya mwisho ni lango la kuingia majira ya Kwaresma. Ni majira ya kuacha kutazama miujiza na kuanza kutazama msalaba. Ni wakati wa kutangaza kuwa injili ya wokovu ni ya neema katika Yesu Kristo kwa njia ya Imani. Kwa hiyo taarifa ya safari ya Yesu sio ya huzuni bali injili ya neema inaanza kufunguka na kujidhihirisha, tunaelekea utukufu wa juu kabisa wa Yesu. Lakini Yesu alitamka jambo ambalo wanafunzi hawakutaka kulisikia kabisa. Yesu anaenda kufa Yerusalemu! Mfalme au Masihi aende kufa.
Ndio hii ndio habari njema, Yesu anaenda mwenyewe, hakukimbia wala kujificha . Huu ndio upendo wa kweli. Alilipa gharama ya wokovu wetu kwa njia ya kifo chake msalabani. Hii inatukumbusha kuwa dhambi ni mbaya sana, hukumu ya Mungu ni ya kweli, lakini neema za Mungu ni kuu zaidi. Yesu anauendea msalaba sio kwamba hakuwa na hofu bali aliishinda hofu bali alikuwa anatii mapenzi ya Mungu, alijua thamani ya safari yake, kumwaga damu ili kumwokoa mwanadamu ambaye alimkosea Mungu akawa hana njia ya kujiosha mwenyewe, alihitaji neema, kulipiwa gharama.
Siku ya tatu atafufuka, tunasikia sauti ya pasaka ndani ya tangazo la kifo. Mateso sio mwisho wala kifo sio mwisho wa ushindi wa Yesu. Hii inatukumbusha sisi kuwa siku ya tatu ipo, huenda tunapitia mateso, maumivu, kukata tamaa Mungu ana siku ya tatu kwa ajili yetu.
Wanafunzi walisikitika kupita kiasi, waliona kama ni mwisho wa ufuasi wao walioutaabikia miaka 3, waliona msalaba bila ufufuo, hata kama walikuwa wamesikia akiusema. Kumbe kuna wakati tunaweza kusikia jambo, lakini tusielewa kabisa lina maanisha nini. Na mara nyingi tunakutana na mambo na hatuyaelewi yanamaanisha nini.
Tunapoingia majira ya Kwaresma tuutazame msalaba kama daraja la kutuvushia kwenye utukufu. Na kwa sababu peke yetu hatuwezi kuvuka, majira ya Kwaresma yanatuita kwenye unyenyekevu na toba. Ni majira yanayotuambia kuwa tuache dhambi ili tuupokee wokovu. Macho yetu yasibakie kwenye vitu tulivyo navyo sasa, bali yatazame kwenye matokeo ya utii ulioanzishwa na Yesu, na kisha ukaja kwetu. Kwaresma inatukumbusha kuwa Yesu alitii mapenzi ya Baba akawa sababu ya wokovu kwa wale watakaotii mapenzi ya Baba. Kipindi hiki cha Kwaresma kinatukomaza zaidi katika kutembea njia ya utii. Basi na tutembee pamoja na Yesu kwenye njia ya utii – kuna kusalitiwa (tena na watu wetu wa karibu), kuna kuteswa, na kuna kuuawa; lakini huo sio mwisho wa habari. Baada ya hayo yote, kuna utukufu na huo ndio utukufu wa kweli. Tukielekeza macho yetu kwenye utukufu huo, mapito na mateso ya wakati huu hayatatuzui kwa lolote. Mungu atujalie kutembea kwa ujasiri katika njia ya msalaba ambao Yesu anauendea.
Amen.