IBADA YA TAREHE 30 JULAI 2023 SIKU YA BWANA YA 8 BAADA YA UTATU

Somo:WEMA WA MUNGU WATUVUTA TUPATE KUTUBU
ZABURI 27:5-10; 2 KOR. 7:7-12;HOSEA 14:1-3*
WIMBO: TMW 149
MAFAFANUZI

1. UTANGULIZI

Ujumbe wa kitabu cha Nabii Hosea uliwasilishwa kwa njia ya kuigizwa katika Maisha ya nabii mwenyewe. Kwa mtazamo wa utumishi na ufuasi haikuwa njia rahisi ya kuwasilisha ujumbe. Nabii Hosea aliagizwa na Mungu kuoa mwanamke kahaba na kuzaa naye watoto. Mungu alisema anafanya hivyo kwa sababu nchi imefanya uzinzi mwingi. Mwanamke aliyemwoa aliitwa Gomeri (Hosea 1:2-3). Hata baada ya kuolewa na Nabii Hosea, Gomeri aliendelea kwenda kufanya uzinzi na wanaume wengine na Hosea aliendelea kumrudisha na hata kumnunua kwa fedha ( Hosea 3:2).

Katika mlango wa tatu nabii anafafanua alichoagizwa na Mungu kufanya na sababu za kufanya hivyo. Aliagizwa ampende mwanamke apendwaye na Rafiki yake naye ni mzinzi, kama vile Mungu awapendavyo wana wa Israel ingawa wamegeukia miungu mingine (Hosea 3:1).

Ndani ya ujumbe wa Hosea kuna onyo kwamba kama Israeli hataacha uzinzi (kuabudu miungu mingine) ataadhibiwa vikali. Lakini kumbuka, adhabu huwa na lengo la kumrekebisha mkosaji. Hukumu ndio shida. Labda mhukumu awe na huruma. Sura zinazofuata Hosea 4-13 zinahusu Mungu na Israeli asiye mwaminifu. Ndani yake sura za 4 na 5 zinazungumzia uzinzi ambao Israeli anaufanya kwa kuabudu miungu mingine. Sura ya 6 Efraimu alirudi kuadhibiwa. Njooni tumrudie Mungu maana yeye amerarua na yeye atatuponya (Hosea 6:1); Sura za 7-12 Israeli (Efraimu) atapona hukumu kama atamrudia Mungu anayempenda. Efraim ni kabila ambako wafalme wengi walitoka. Sura ya 13 Israeli atahukumiwa sasa na sura ya 14 inaonyesha kuwa Israeli ataokolewa baadaye.

Ukijumlisha ujumbe wa Hosea unakuwa tabia yao ya kutokuwa waaminifu ndio sababu ya hukumu itakayokuja. Hii sura ya mwisho ni ya matumaini kwa taifa lililotubu. Hosea aliitwa kuhudumu katika taifa lililochanganyikiwa na limepoteza maadili na uchaji. Alipewa wajibu mkubwa mno wa kuoa kahaba na yeye kubaki mwaminifu katika ndoa yake kama Mungu alivyo hata kama mke wake alikwenda kwa wanaume wengine.

Fikiria tu njia hii ya kuwasilisha uasi ambao umefanywa na wana wa Israeli angepewa mchungaji mmojawapo leo. Kwanza, yeye mwenyewe angesema hiyo sio sauti ya Mungu na wale wanaoogonzwa naye wengi wangetia mashaka kama kweli ni Mungu ameruhusu hilo.

2. HOSEA 14:1-3

Sura hii ya mwisho ya kitabu cha Hosea inakuja na kitu cha pekee baada ya kutupitisha kwenye ujumbe wa hukumu. Anakuja na ujumbe wa rehema. Rehema ni msaada unaoambatana na huruma. Mungu mwenyewe anatoa maelekezo namna ya kufanya toba ili kumrudia Mungu. Anaelekeza ili kufikia toba nini cha kusema na nini cha kufanya. Ujasiri wa kutubu unajengwa na utayari wa Mungu kuwapokea wenye dhambi wanaporudi. Mungu anasema nitawaponya kurudi nyuma kwao, nitawapenda kwa ukunjufu wa moyo kwa maana hasira yangu imemwacha (Hosea 14:4,8). Pia zipo faraja kubwa ambazo ameziandaa kwa ajili ya Israeli anayetubu (Hosea 14:5,7). Ujumbe unahitimishwa kwa swali kwamba ni nani aliye na hekima na atayafahamu mambo haya? Na nani mwenye busara atakaye yajua? Ni maswali yanayotuhusu sisi sote katika ukweli wa kuyapokea haya (Hosea 14:9).

Hosea 14:1 Israeli mwenye dhambi anaitwa kurudi (kutubu).

Kumbe kila mtu anahitaji ujumbe wa toba hata walio ndani ya agano kama Israeli. Kwa hiyo hata Wakristo ndani ya kanisa wanahitaji ujumbe wa toba kila siku. Israeli mrudie Mungu wako kwa maana umeanguka kwa sababu ya uovu wako. Na kurudi ni kurejesha uhusiano (fellowship) uliopotea au uliovunjika. Ulipotea au kuvunjika namna gani? Ni pale walipoanguka au kujikwaa kwa sababu ya kuabudu miungu mingine na kumwacha Mungu aliye hai ambaye anawapenda. Ndio picha ya ndoa ya Hosea na Gomeri. Wanarudi kwa njia gani? Ni kwa kutubu na kutengeneza.

Hosea 14:2 Chukueni maneno pamoja nanyi

Wanaporudi wameelekezwa maneno ya kwenda nayo ambayo ni kumwambia Bwana: Ondoa maovu yote, uyatakabali yaliyo mema. Na hivyo ndivyo mtakavyotoa sadaka za midomo yetu kana kwamba ni ng’ombe.
Wanapomrudia Bwana hawaendi kimya kimya na lazima waende kama Bwana anavyotaka na anavyoelekeza. Hataki wafikiri tu mioyoni na kujisikia hatia ya dhambi bali wakiri maneno hayo kwa midomo yao. Wamwambie Mungu kwamba tunakupenda na kwamba tumekukosea. Hata katika mahusiano yetu mfano ya mume na mke huwa ina nguvu kumwambia mwenzi kwamba unampenda, hata kwenye viapo vya ndoa wenzi huwa wanakiri kwa midomo yao kueleza upendo wao na kujitoa kwao katika ndoa. Katika viapo hivyo tunabeba maneno pamoja nasi. Mtume Paulo katika Warumi 10:8-10 anasema mtu kwa moyo huamini hata kupata haki na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.

Je, tunachukua maneno gani pamoja nasi?

Hayo maneno sahihi ya kwenda nayo tunayapata kutoka kwa Mungu mwenyewe katika neno lake. Mfano Mdo 3:19 tunaambiwa tubuni basi mrejee, ili dhambi zenu zifutwe. Na Mathayo 3:2 Yohana alihubiri tubuni mwache dhambi zenu. Na Yesu alianza huduma yake kwa kuagiza toba, Mathayo 4:17 tubuni.. Upo umuhimu wa kukiri maasi yetu kwa midomo yetu. Zaburi 32:5 c; Nalisema nitayakiri maasi yangu kwa Bwana. Katika toba kuna umuhimu mkubwa wa mtu kukiri kosa alilofanya. Katika mifumo mingi ya kanisa wapo watu waliopewa wajibu wa kuwasikiliza wengine wanapotengeneza mambo yao na Mungu. Kuna wachungaji waliokula kiapo cha kufanya hivyo. Kuna watu wanafundisha kuwa inatosha kumwambia Mungu makosa yako, sawa lakini kuna mahali hali na hatia ya dhambi haiishi hadi mtu amekiri kwa midomo yake. Shida ni pale ambapo huduma imeingiliwa na watu ambao hawana dhamana ya kufanya hilo na kusimama kama mawakili wa siri za Mungu au wale wenye dhamana wanapokengeuka na kuharibu huduma. Lakini ukweli utabaki kuwa katika toba upo umuhimu wa kukiri kwa midomo yetu.

Tunamwambia nini Mungu katika toba yetu?

Ondoa maovu yote na utupokee kwa rehema zako. Hata katika sala ya Bwana Yesu alitufundisha kukiri makossa yetu mbele za Mungu ili atusamehe. Tunaporudi kwa Mungu lazima tunyenyekee mbele zake na kukubali kwamba tumekosa, tumefanya dhambi na tunahitaji msaada wake. Tunamhitaji yeye tu hatuna lolote la kufanya Zaidi ya kujiachia mikononi mwake.

Na ndivyo tutatoa sadaka ya midomo yetu kama sadaka ya ng’ombe. Maana yake maneno yetu ya toba na sifa mbele za Mungu ni sadaka ya kuteketezwa mbele za Mungu. Katika toba hiyo tutakiri wazi na kutengeneza mambo matatu:
(a) Kukataa kutegemea mataifa ya kigeni (Ashuru). Mungu pekee yake ndiye mwokozi wetu.
(b) Tutaacha kutegemea uwezo wa kivita kama kutegemea farasi (Zaburi 20:7).
(c) Tutakataa kutegemea sanamu, kazi za mikono yetu bali tutamtegemea Mungu pekee yake.
Wito wa nabii Hosea katika kifungu hiki (Hosea 14:1-3) ni kuwaita Israeli kurudi kwa Mungu kwa moyo wa dhati. Amewapa maneno ya kuomba wanaporejesha uhusiano wao na Mungu. Mwana mpotevu katika Luka 15:11-32 yeye alipanga maneno ya kusema anaporudi nyumbani kwa baba.
Kitabu cha Hosea kinahusu mambo ya dhambi na hukumu lakini pia upendo na huruma za Bwana kwa watu wasiostahili kama ambavyo Gomeri hakustahili kuwa mke wa nabii. Na Upendo huo wa Mungu umeonyeshwa kwa njia ya ndoa hiyo ya nabii Hosea na mwanamke Gomeri. Ni picha inayoumiza moyo kwa mtazamo wa kibinadamu, je, kwa Mungu mtakatifu sio zaidi?

3.WEMA WA MUNGU WATUVUTA TUPATE KUTUBU

Kutokana na mafunzo ya kitabu hiki utagundua kuwa kumbe Mungu anapomtendea mema huyu mwanadamu aliye mwovu sio kwamba anataka aendelee kutenda uovu bali anataka avutwe na upendo wa Mungu na hivyo aweze kugeuka na kujinyenyekesha kwa toba.
Mungu atujalie tutambue hilo na kutumia neema hiyo ya nguvu ya toba.
Amen.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *