IBADA YA TAREHE 23 JULAI 2023,SIKU YA BWANA YA 7 BAADA YA UTATU

Somo:UCHAGUZI WA BUSARA
ZABURI 37:1-8; LUKA 10:38-42
MATENDO 6:1-6*
WIMBO: TMW 422
MAFAFANUZI

1. UTANGULIZI
Hadi wakati huu wafuasi wa Yesu walikuwa wachache sana, lakini siku ya Pentekoste waliongezeka waumini elfu tatu (3,000). Kwa mujibu wa mwandishi wa Kitabu cha Matendo, Mungu aliongeza wanafunzi kila siku (Mdo 2:47). Mitume wakaweka nguvu zao katika kuhubiri, kufundisha, kuomba na kuombea wagonjwa (Mdo 3:1-26; 5:12-15), wakaongezeka wafuasi wengine elfu tano (Mdo 4:4). Kanisa la mwanzo lilikuwa vizuri sana katika kutunza takwimu hadi lilijua watu wangapi wameokoka, na lini.
Kanisa lilifanya mambo yote kuwa shirika. Likatunza wajane na wahitaji wengine (diakonia). Kwa vile mitume waliweka kipaumbele na mkazo wao katika kuhubiri na kuomba, suala la usimamizi wa mambo ya huduma (diakonia ). Walitambua kuwa kipaumbele ni neno na maombi lakini suala la diakonia bado lilionekana kuwa muhimu. Ndio maana kulipojitokeza manung’uniko kanisa lilichukua hatua haraka sana kwani lilijiona kuwa lilipaswa kufuata mfano wa Yesu wa kuwahudumia wahitaji, lakini pia lilifahamu kuwa hisia za ubaguzi ni hatari zinaweza kuligawa kanisa.
2.WATUMISHI SABA WAWEKWA KUJIBU MANUNG’UNIKO YA KUNDI LA WAYAHUDI WA KIYUNANI (MDO 6:1-7)
Kifungu kinachotangulia somo letu na kinachomalizia mlango wa tano (Mdo 5:42) kinasema: Na kila siku ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema ya Yesu kwamba ni Kristo. Na kutokana na kazi hiyo kanisa lilikua na kuongezeka kila siku. Na tatizo tunalokutana nalo katika somo letu linaashiria kwamba kasi ya ukuaji wa kanisa ilikuwa kubwa mno hadi wakashindwa kutawala mabadiliko hayo makubwa, wakashindwa kutoa huduma kwa watu kama inavyotakiwa. Kukatokea manung’uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwamba wajane wao kwamba walisahauliwa katika huduma ya kila siku (daily service au Kiyunani kathemerinos diakonia).
Inaonekana kanisa lilikuwa limeweka mpango wa kuwasaidia wajane kupata mlo wa kila siku. Lakini kukatokea manung’uniko toka Wakristo ambao ni Wayahudi wa Kiyunani kwamba walisahauliwa kwenye mgawo wa chakula. Kwamba ni kweli au ilikuwa hisia tu hatujui. Kitu ambacho kinafahamika ni kwamba waliitisha mkutano wa jamii ya waaminio na kuwashirikisha changamoto hiyo na kutoa mapendekezo namna ya kulitatua. Kwa kuwa walikuwa wameweka vyote shirika (Mdo 4:34) inaonekana shida haikuwa kukosekana kwa chakula bali utaratibu wa kugawa. Lilikuwa suala la utawala na usimamizi.
Wale 12 wakaitisha mkutano na kushirikisha watu lile tatizo na pia wakaelekeza nini kifanyike. Hapa tunaona uamuzi wa busara kusikiliza tatizo na kulichukulia hatua mara moja. Wakagundua kuwa tatizo lile ni la utawala, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani (Mdo 6:2). Mitume walijua nini walikabidhiwa na Bwana Yesu (Mathayo 28:19-20; Mdo 1:8) walipewa wajibu wa kuhubiri na kufundisha neno na sio kugawa chakula au kufanya mambo ya utawala wa chakula. Haina maana kwamba kazi hiyo sio muhimu bali waliangalia vipaumbele vya wito wao na wajibu wa msingi.
Baadaye tunajifunza kuwa Kanisa lilifanya kazi kufuata vipawa mbali mbali ambavyo Mungu amevigawa ndani yake (Rumi 12:12-26; 1Kor. 12:27-31 na Efeso 4:11-16). Ni vema na ni muhimu kuheshimu vipawa ambavyo Mungu ametupa na kuwa waaminifu kwa wito wetu. Ingekuwa kosa kwa Mitume kuacha kuhubiri wakaanza kusimamia chakula. Mitume walijitambua kuwa hawakuitwa ili wawe kila kitu katika kanisa.
Mitume wakaelekeza kuwa basi chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili (Mdo 6:3). Wakataja sifa za hao wasimamizi au wadiakonia. Walitakiwa kushuhudiwa na watu kuwa na sifa ya wema, vinginevyo wasingeweza kuhudumu kwa ufanisi. Walipaswa kujawa na Roho Mtakatifu. Kazi yo yote kanisani inahitaji watu wenye Roho Mtakatifu na hekima za Mungu. Ushauri huu unafanana na ushauri ambao Yethro aliutoa kwa Musa (Kutoka 18:18-22). Kwa hiyo sifa hizo tatu za kushuhudiwa wema, kujawa Roho na hekima zinawahusu Makatibu wakuu, Watunza Hazina, watu wa utawala, madereva, makarani, nk. Mitume walisema watu wenye sifa hizo ndio wakabidhiwe jukumu hilo.
Mitume wakaeleza ni nini wao watajishughulisha. Wakasema sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile neno (Mdo 6:4). Wanajibainisha kuwa kipaumbele kwao ilikuwa maombi na neno la Mungu. Kwa hiyo walitoa muda wa kutosha kwa ajili ya maombi na neno. Uchaguzi wa busara ni kujua vipaumbele na kuvitekeleza.
Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote (Mdo 6:5a). Hapa ni kwamba kanisa zima lilifurahi sio tu wale Wayahudi wa Kiyunani ambao walinung’unika. Wote walifurahi kupona kwa mwili wa Kristo ambao ulikuwa umejeruhiwa kwa sehemu mojawapo ya viungo kujeruhiwa. Hapakuwa na ushindani wowote hoja ilipokelewa na kutengenezewa suluhu ya pamoja.
Wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, Filipo na Prokoro,na Nikanoni, na Timoni, na Permena na Nikolao mwongofu wa Antiokia (Mdo 6:5b). Hapa inaonekana Mitume hawakutaja mtu, waliacha mkutano wenyewe uchague watu. Na kwa kuangalia majina yote saba yana asili ya Kiyunani kwa hiyo ni kusema kama Wadiakonia wote walitoka upande wa wale walioonekana wajane wao kupunjwa. Hili inaonekana walilifanya kwa upendo kabisa. Kati ya hao Stefano ameelezewa kipekee na baada ya hapo tumesikia habari za Stefano mfia dini ila hatujasikia habari za wale waliobaki. Na kwa vile hatujasikia tena manung’uniko inawezekana kazi yao ya kusimamia utaratibu wa chakula ilifanikiwa vizuri.
Wakawaweka mbele ya Mitume (Mdo 6:6a). Baada ya wale watu saba kuchaguliwa ni kama waliwekwa mbele ya mitume ambao kwa wakati ule waliokuwa ndio mamlaka ya juu katika kanisa. Waliwekwa kama ili wawathibitishe. Hawa Mitume kama viongozi wa juu katika kanisa bado walikuwa wanafikika kwa urahisi ndio maana walielezwa tatizo lililo wakabili. Ni busara kufikika ili matatizo yawasilishwe mapema.
Mitume wakawaombea na kuwaweka mikono yao juu yao (Mdo 6:6b). Waliwekewa mikono ili kutumwa kwa kazi maalum (Mdo 13:3; 2 Timotheo 1:6). Waliwekewa mikono kuthibitisha uchaguzi ule na kuwatuma kazini. Hata nyakati za sasa katika kanisa watumishi wanawekewa mikono na kufanyiwa maombi wanapoingizwa katika kazi mbali mbali.
Neno la Mungu likaenea na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu, jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile imani (Mdo 6:7). Kama Mitume walivyosema kwamba wao watadumu kuhudumu neno na katika maombi, matokeo yake kanisa likakua haraka sana pale Yerusalemu na makuhani ambao walikuwemo maeneo ya ibada ambapo Mitume walihubiri nao wakaamini na kutii imani. Kwa hiyo mahubiri na mafundisho ya mitume yaliwaongoa hata Makuhani.
3.UCHAGUZI WA BUSARA
Jambo kubwa katika somo letu limekuwa ni juu ya manung’uniko yaliyotokea katika kanisa la mwanzo. Kundi moja lilijisikia kubaguliwa. Kwa busara na kufikika kwa Mitume walifaulu kugundua kuwa hawapo salama kwa sababu kuna kundi linanung’unika. Leo kuna manung’uniko mengi katika jamii, katika familia, katika kanisa na katika nchi yetu. Inahitajika busara ya viongozi katika maeneo hayo kutopuuza na wachukue hatua ya haraka. Na mahali pengine manung’uniko yanatokea kutokana na hisia za kutotendewa haki au kubaguliwa. Ili kuondoa hisia wataalam wa sheria walisema, sio tu kwamba haki itendeke katika jamii bali ionekane kuwa inatendeka.
Katika kutafuta suluhu la tatizo lililolikabili kanisa la mwanzo tunakutana na uchaguzi wa busara ufuatao:
✓Kwanza, kusikiliza manung’uniko na kuyafanyia kazi hata kama hayana msingi ni jambo la busara.
✓Pili, katika kutatua tatizo mitume walishirikisha watu, huo ni uongozi shirikishi.
✓Tatu, Mitume walielekeza sifa za watu wa kuchaguliwa kuwa wawe wenye ushuhuda mzuri, waliojawa na Roho na wenye hekima.
✓Nne, Mitume waliacha watu wachague wenyewe na sio kuwashinikiza.
✓Tano, Mitume walifahamu vizuri mno wito wao na vipaumbele. Wakaweka nguvu zao katika maombi na neno. Kusimamia chakula na fedha sio kwamba hazikuwa kazi muhimu bali waliangalia vipaumbele na kugawana vipawa.
Katika mambo haya matano mara nyingi viongozi wengi nyakati zetu yamekuwa changamoto. Hawasikilizi manung’uniko hadi yanageuka kuwa migogoro, hata wakitaka kutatua wachache wanashirikisha watu na wanafanikiwa, wale wanaofanya bila kushirikisha watu hawafaulu. Jambo jingine la busara ni kuzingatia sifa za wale wanaopewa kufanya kazi ndani ya kanisa. Na suala la mwisho ni juu ya vipaumbele. Ni kiasi gani kazi zetu tunazifanya kufuata vipaumbele. Kwa mfano watumishi wengi wa madhabahuni tumepata shida kuweka katika uwiano shughuli za maendeleo na uchumi, fedha na mipango na suala la maombi na neno. Mungu atusaidie sana.
Amen.
Ev.john -0768386606

One thought on “IBADA YA TAREHE 23 JULAI 2023,SIKU YA BWANA YA 7 BAADA YA UTATU”

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *