IBADA YA TAREHE 22 FEBRUARI 2026* SIKU YA BWANA YA 6 KABLA YA PASAKA (INVOCAVIT – MUNGU ANAITA NAMI NAITIKA)

SOMO:KATIKA YESU KILA JARIBU LINA MLANGO WA KUTOKA
ZABURI 139:11-16;
MATHAYO 4:1-11
*SOMO LA MAHUBIRI: DANIELI 3:19-23*
WIMBO: TMW 86
*UTANGULIZI*
Nebukadreza mfalme wa Babeli aliishinda Yerusalemu na kuwachukua watu mateka wakiwepo kutoka katika nyumba ya kifalme, huu ulikuwa wakati wa Mfalme Yehoyakimu wa Yuda, pia vyombo vya nyumba ya Bwana vilichukuliwa hadi Babeli. Hii ilikuwa hukumu ya Mungu kwa uasi wa ufalme wa Yuda. Kwa upande mwingine huu ulikuwa mwanzo wa mpango wa Mungu ndani ya uhamisho (Danieli 1:1-2). Mateso na majaribu hayamaanishi kwamba Mungu hayupo. Mfalme Nebukadreza akamwagiza Ashpenazi Mkuu wa matoashi amtafutie vijana wa Kiebrania wenye vinasaba vya kifalme, wasio na mawaa, wazuri wa uso, wajuzi wa hekima, werevu kwa sababu ya maarifa yao, wenye kufahamu elimu, watakaoweza kusimama katika jumba la kifalme. Ili wafundishwe lugha ya Wakaldayo, elimu ya kifalme, na utamaduni mpya. Vijana hawa wanne hata majina yao yalibadilishwa kama jaribio la kubadili utambulisho wao wa kiimani lakini ilishindikana walibaki na Imani yao (Danieli 1:3-7). Vijana hao ni: Danieli – Belteshaza Hanani – Shadraka Mishaeli – Meshaki Azaria – Abednego Hawa vijana walionesha msimamo usiokuwa wa kawaida walikataa kula chakula cha kifalme walichoagizwa walishwe miaka mitatu wao wakala mtama na maji na afya zao zikawa nzuri kuliko wale vijana waliokula chakula cha mfalme. Mungu aliwapa neema na hekima na mwisho wa siku walipoingizwa mbele ya mfalme kwa usaili walionekana kuwa bora mara kumi zaidi ya waganga na wachawi waliokuwa katika ufalme wake (Danieli 1:-20). Ilitokea kwamba mfalme aliota ndoto ambayo ilifadhaisha roho yake na usingizi kumwacha. Alitoa amri ya kuitwa kwa waganga, wachawi, wasihiri na wakaldayo ili watoe tafsiri ya ndoto ambayo alikuwa ameisahau. Wakaldayo wakajibu na kusema kuwa Hapana mtu duniani awezaye kulionesha neno hili la mfalme kwa maana Hapana mfalme wala bwana aliyetaka neno kama hili. Ni neno la ajabu analotaka mfalme, hakuna awezaye kumwonesha mfalme neno hilo ila miungu wasio na kikao Pamoja na mwenye mwili. Mfalme akakasirika mno akatoa amri ya kuua wenye hekima wote wa Babeli (Danieli 2:1-12). Wenye hekima wakawa wanatafuta kuuawa na Danieli na wenzake ambao hawakuwepo wakati wale wengine wanashindwa akawa anawatafuta Pamoja na wenzake ili wauawe. Danieli akamuuliza Arioko Akida wa walinzi wa mfalme aliyetumwa kuwaua, akasema, mbona amri ya mfalme inau kali hivi? Akaomba aingie kwa mfalme na akaomba apewe muda wa Kwenda kutafuta hiyo tafsiri. Danieli akawapasha Habari wenzake watatu kwamba waombe rehema na kupewa tafsiri au siri ya ile ndoto. Usiku Danieli akapewa ile ndoto ambayo mfalme aliota Pamoja na tafsiri yake. Mfalme Aliona sanamu kubwa. Kichwa cha dhahabu – Babeli (Ufalme wa Nebukadreza). Kifua na mikono yake ya fedha – Ufalme unaofuata. Tumbo na viuno vyake vya shaba – ufalme mwingine Miguu ya chuma nyayo zake nusu chuma na nusu udongo – Falme zinazogawanyika. Maana yake falme hizi ni za muda na dhaifu. Jiwe lililochongwa bila mikono, liliipiga sanamu miguu ikavunja vipande vipande huu ni ufalme wa Mungu wenye nguvu na utadumu milele (Danieli 2:13-45). Mfalme Nebukadreza akamtukuza Mungu akampa Danieli cheo cha kuwa mkuu juu ya Uliwali wote na mkuu wa wote wenye hekima wa Babeli na Danieli akawaombea nafasi wale wenzake watatu (Danieli 2:46-49). Tunapoanza na masilimulizi ya sura ya tatu inaonekana kuwa mfalme Nebukadreza aliazimia kupinga maelekezo ya Mungu ambayo yalitolewa na Danieli katika tafsiri ya ndoto. Aliamua kutengeneza sanamu ya dhahabu tupu kama kuashiria kuwa ufalme wake hautakoma kinyume na ujumbe wa ndoto. Nebukadreza aliamuru watu wote waabudu sanamu ile na kutofanya hivyo ilitafsiriwa kama kosa la uhaini (treason). Watu wote walitii isipokuwa watatu (Shadraka, Meshaki na Abednego). Kufuatia habari zilizopo sura ya pili, Danieli alipandishwa cheo na hivyo akawa anatumika ikulu, kwa hiyo hakujumuika nao. Huu ulikuwa mtihani wao na Danieli alipewa mtihani wake peke yake baadaye (Danieli 6). Inaonekana watu walikuwa wanawafuatilia wakagundua kuwa hawa jamaa wamegoma kuabudu sanamu, wakapeleka taarifa kwa mfalme Nebukadreza. Inaonekana kulikuwa na wivu wa kisiasa kwani hawa wageni walipewa nafasi za utawala. Nebukadreza hakutaka kuwachukulia hatua kwa maneno ya kusikia akawaita na kuwahoji. Je, ni kweli mmekataa kuabudu sanamu? Akawapa nafasi ya kufanya hivyo na kwamba wakikataa watatupwa kwenye tanuru la moto ili aone ni mungu yupi atakaye waokoa na mkono wake na pia na tanuru la moto. Na hapa ndipo alipokosea kumhusisha Mungu katika hoja zake. Wakamjibu kuwa hawakuwa na haja ya kujitetea, kosa wanalijua lakini Mungu wanayemtumikia atawaokoa na tanuru na mkono wa mfalme. Wakasema wazi kuwa hawakuwa tayari kutumikia miungu ya Nebukadreza wala kuabudu sanamu yake (Danieli 3:1-18). Ndipo linafuata somo letu la mahubiri (Danieli 3:19 -23). Mfalme Nebukadreza akastaajabu, akainuka haraka, akauliza kuwa je, hatukutupa watu watatu wakiwa wamefungwa? Mbona anaona watu wanne wamefunguliwa, wanatembea Katikati ya moto na hauna madhara na yule wa nne ni mfano wa mwana wa miungu. Akawaita Shadraka, Meshaki na Abednego kuwa ni watumishi wa Mungu aliye juu kuwa watoke nje. Nebukadreza akamhimidi Bwana na kuweka amri kwa kila kabila za watu, kila taifa na kila lugha kuwa yeyote atakaye nena neno lolote lisilopasa juu ya huyo Mungu wa Shadraka, Meshaki na Abednego atakatwa vipande vipande na nyumba zao kufanywa jaa kwa kuwa hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii. Kisha akawapandisha vyeo katika wilaya ya Babeli (Danieli 3:24-30). 2. *DANIELI 3:19-23 HASIRA YA MFALME NA MOTO MKALI DHIDI YA SHADRAKA, MESHAKI NA ABEDNEGO* Shadraka, Meshaki na Abednego walikataa kuabudu sanamu ya Mfalme Nebukadreza kwa sababu ya uaminifu wao kwa Mungu mmoja, aliye hai na ndiye pekee anapaswa kuabudiwa. Mfalme akawatisha juu ya uamuzi wao na kwamba angewachoma moto. Bado walikaza uamuzi wao na kutamka wazi kwamba moto hauna nguvu juu ya nguvu za Mungu. Mfalme kwa hasira akaamuru tanuru lichochewe mara saba kuliko kawaida. Hasira ya Nebukadreza inadhihirisha uasi wa mwanadamu dhidi ya Mungu. Hasira ya mfalme ilitokana na ushuhuda wa kishujaa uliotolewa na wale vijana watatu. Kabla hawajatoa msimamo wao mkali juu ya Imani yao katika Mungu aliye hai alikuwa akiwasemesha kama watoto wake. Hawakuona aibu kumshuhudia Mungu wao. Mfalme akatumia tanuru ambayo inasimama kama ishara ya hukumu, mateso, mauti. Kwa hakika tunaweza kuona kivuli cha msalaba katika tukio hili. Kwani hata Yesu alihukumiwa na mamlaka za dunia hii kama akina Shadraka, Meshaki na Abednego walivyohukumiwa. Baada ya moto huo mkali kuandaliwa walitafutwa vijana wenye nguvu, wakawafunga watumishi wa Mungu na kuwatupa katika tanuru la moto, wale waliowabeba Shadraka, Meshaki na Abednego moto uliwalamba wenyewe wakafa. Mle ndani wakaonekana akina Shadraka, Meshaki na Abednego wakiwa huru hawajafungwa tena. Mfalme alishangaa mno kwani halikuwa tukio la kawaida. Katika tafsiri ya toleo la Septuagint inasema, mfalme alishituka kusikia wale vijana wanne wakiimba nyimbo za sifa ndani ya tanuru. Moto ulikula Kamba zilizowafunga lakini haukugusa nguo zao wala nywele wala hata harufu tu ya moto hawakuwa nayo. Mle ndani akina Shadraka, Meshaki na Abednego hawakuwa peke yao walikuwa na mtu wa nne aliyeonekana kuwa ni mwana wa Mungu. Kumbe Yesu aliingia nao katika tanuru. Sio lazima Mungu akaepushe na majaribu au mateso wakati mwingine anakwenda na wewe, usiogope hupo peke yako. Hatuna uhakika kama akina Shadraka, Meshaki na Abednego walijua kuwa wapo Pamoja na Yesu mle ndani ya tanuru ya moto. Kwa hiyo tuwe tunaona au hatuoni Yesu yupo Pamoja nasi. Mfuasi wa Kristo pia ana tanuru za aina mbali mbali ambazo anakutana nazo katika maisha. Kuna tanuru ambazo mtu mwenyewe anajitengenezea, zipo ambazo zinatengenezwa na Shetani na nyingi zinaandaliwa na Mungu. Kwa hiyo Mungu anaweza kutuokoa kutoka katika majaribu au akatuwezesha kubeba au kushinda jaribu hilo.
3.*KATIKA YESU KILA JARIBU LINA MLANGO WA KUTOKA*
Habari za vijana wanne Danieli, Shadraka,Meshaki na Abednego zinatuonesha kuwa vijana hawa walikuwa Hodari na wenye ufanisi mkubwa tangu kuitwa kwao. Ufanisi wao haukuwa kwa sababu ya elimu tu wala nafasi zao nzuri serikalini bali ulitokana na msingi wa kiroho ambao uliongoza maisha yao yote. Ushindi wao juu ya majaribu haukupatikana katika siku moja bali ulishuhudia aina ya watu walivyo na jinsi walivyoishi na Mungu. (a) Walikuwa wameandaliwa toka nyumbani na mfalme alitafuta watu wenye sifa. (b) Walikuwa na uamuzi moyoni juu ya kumtii Mungu. Danieli na wenzake waliazimia moyoni kutojitia unajisi na vyakula vya mfalme hata kama vilionekana kuwa vyenye sifa wao wakala mtama na kunywa maji (Danieli 1:8). Kwa hiyo mafanikio yao yalianza moyoni kwa uhusiano sahihi na wauaminifu na Mungu. (c) Walidumisha maisha ya utakatifu na hofu ya Mungu Katikati ya maisha ya kipagani. Shadraka, Meshaki na Abednego waliposhurutishwa kusujudia sanamu walikataa hata walipotishwa na tanuru la moto. Walichagua kuwa waaminifu kwa Mungu na kuuacha usalama wa maisha yao mikononi mwa Mungu (Danieli 3). (d) Walikuwa watu wa maombi na kumtegemea Mungu kila siku. Maisha ya ushindi hayaanzi na mbinu bali na uhusiano. Danieli alipata ushindi kwa sababu aliishi mbele za Mungu kila siku (Danieli 6:10). Danieli hakuanza kuomba baada ya tishio bali aliomba kama ilivyokuwa desturi yake na akaendelea hata baada ya amri ya kutokuomba kutangazwa. Hatuanzi kuomba baada ya kuingia majaribuni tunahitaji kuishi maisha ya maombi. (e) Mungu alisimama upande wao. Moto haukuwaunguza (Danieli 3) na simba hawakumwangamiza Danieli (Danieli 6). Mungu hatuzuii tusipitie majaribu bali anapita nasi katika majaribu. Alienda na akina Shadraka ndani ya tanuru la moto, alienda na Danieli ndani ya tundu la simba na kuwafumba vinywa vyao. Mungu hakungoji nje bali anaenda Pamoja nawe. Majaribu ni njia ya kuuendea ushindi. Ndio maana wapo ambao hufika kwenye ushindi na wengine hurudia njiani. (f) Walitumia ujuzi na karama zao kwa utukufu wa Mungu. Hawa vijana wanne walikuwa na hekima, maarifa na nafasi za juu katika serikali kule Babeli lakini walielekeza utukufu kwa Mungu sio kwao. Katika somo letu tunajifunza kuwa Kristo yupo na watu wake katika moto. Yesu hatuokoi akiwa mbali kama mtazamaji bali anaingia katika mateso, anaingia mwenyewe katika tanuru la moto uliokolezwa mara saba. Majira haya tumeanza safari ya Kwaresma tangu jumatano ya majivu (18/02/2026), ni majira ya kutafakari mateso ya Bwana Yesu, kutubu dhambi na kujifunza juu ya tumaini la msalaba. Neno letu limetupeleka Babeli kwenye tanuru la moto ambako vijana wale watatu walikataa kusujudia sanamu, wala miungu ya Wakaldayo. Walikuwa tayari kupitia mateso hata kifo kwa ajili ya Imani yao. Kipindi hiki cha kwaresma tunamwona yule Yesu ambaye alikuwa na wale vijana ndani ya tanuru la moto, anauendea msalaba kwa ajili ya ukombozi wetu wanadamu. Kuonekana kwake ndani ya tanuru ulikuwa udhihirisho wa Yesu kabla hajazaliwa katika mwili. Uwepo wa Yesu ndani ya tanuru la moto ni ujumbe kwamba Mungu hayuko mbali na mateso ya watu wake. Haangalii toka toka mbinguni bali alifanyika mwili na kupita nasi katika mateso. Mungu anaingia ndani ya moto wa dhambi ambazo zilitutesa, hii ndio injili ya Kwaresma, ukombozi kwa njia ya msalaba. Pamoja na Yesu ndani ya tanuru akina Shadraka walikuwa huru wakitembea, hawajafungwa na wala hawakuungua. Moto upo lakini hauwezi kutuangamiza, kifo kipo lakini Yesu ni mshindi w amauti, mateso yapo lakini sio mwisho kwa sababu Yesu yumo ndani ya moto Pamoja nasi. Ujumbe wa msalaba unasema, Yesu huokoa si kwa kuondoa mateso kwanza, bali kwa kuwa Pamoja nasi ndani yake. Tukiangalia masomo yetu yote matatu tuliyopewa katika kalenda Zaburi 139:11-16; Mathayo 4:1-11 na Danieli 3:19-23 yote yanatutaka tuelekeze macho yetu kwenye siri ya ushindi wa Mungu Katikati ya giza, majaribu na moto. *Zaburi 139:11-16* Mungu alimwona Daudi na kumuandaa kabla ya vita. Hakuna giza linaloweza kumficha mtu mbele za Mungu. Mungu alimuumba mtu kwa jinsi ya ajabu tangu tumboni na kupanga siku zake zote. Kabla ya jaribu halijaja Mungu tayari anajua na ameandaa ushindi. Tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu kiasi kwamba maarifa hayo hatuwezi kuyafikia na kuyaelewa. Kwa hiyo kwa kufuata Zaburi yetu hatuingii vitani, majaribuni peke yetu bali tunaingia tukiwa tunajulikana na Mungu. Mungu hutuandalia mlango wa kutoka kabla hatujaingia. Yeye hutangaza mwisho tangu mwanzo (Isaya 46:10). *Mathayo 4:1-11.* Yesu anajaribiwa jangwani, tena alipelekwa na Roho Mtakatifu. Alipata majaribu matatu: Jaribu la mwili, mkate; jaribu la kujionesha aruke kutoka hekaluni na jaribu la mamlaka na umiliki bila msalaba. Yesu alichukua mamlaka kwa njia ya msalaba na kumiliki vyote (Waefeso 1:18-23). Katika majaribu hayo yote Yesu alishinda kwa Neno la Mungu kila mara akisema, Imeandikwa … Kama Yesu alishinda kwa neno, na sisi hatuwezi kushinda kwa nguvu zetu bali kwa Neno ambalo pia ni Yesu mwenyewe. Katika somo la Danieli *(Danieli 3:19-23)* tumeona wale vijana wakiwa na mtu wa nne ndani ya moto. Mungu haji kabla ya jaribu, huingia ndani ya jaribu Pamoja nasi. Kumbe moto ambao ulipanga kutuangamiza unageuka kuwa mahali pa ufunuo wa uwepo wa Mungu na mahali pa Mungu kutukuzwa na kuabudiwa na watu wote.
Uwe na Kwaresma nje

MAHUBIRI YA IBADA YA JUMATANO YA MAJIVU TAREHE 18/02/2026

Wazo:RARUENI MIOYO YENU
Yoeli 2:15-20*
*UTANGULIZI*
Wapendwa katika Kristo Yesu, neema na amani zitokazo kwa Mungu Baba na Bwana wetu Yesu Kristo ziwe nanyi nyote. Amina.
Leo tunaingia katika kipindi cha Kwaresma, tukianzia Jumatano ya Majivu. Ni kipindi cha kutafakari mateso ya Bwana wetu Yesu Kristo, kujichunguza, kutubu, na kurejea kwa Mungu kwa moyo wote.
Neno la Bwana kupitia nabii Yoeli linatuita kwa sauti kuu:
“RARUENI MIOYO YENU.”
Siyo kurarua mavazi, siyo ishara za nje tu, bali ni mabadiliko ya ndani kabisa.
2. *Ufafanuzi (Yoeli 2:15–20)*
Nabii Yoeli aliishi wakati ambapo taifa la Israeli lilipitia janga kubwa – uvamizi wa nzige uliharibu mazao, uchumi ukaporomoka, njaa ikaenea. Hali hii haikuwa tu tukio la kawaida la asili, bali ilikuwa ishara ya kiroho – watu walikuwa wamemwacha Mungu.
Ndipo Mungu akatoa wito:
“Pigeni tarumbeta Sayuni” – Tangazeni mkutano mtakatifu.
“Kusanyeni watu, watakaseni mkutano.”
Hata wazee, watoto, wachanga, na hata wanandoa waliokuwa kwenye chumba cha harusi waliitwa kuja mbele za Mungu.
Kwa nini?
Kwa sababu tatizo lilikuwa la kitaifa na suluhisho lilikuwa toba ya pamoja.

3. *UFAFANUZI WA MADA: “RARUENI MIOYO YENU”*
Katika utamaduni wa Kiyahudi, mtu alipokuwa na huzuni au toba, alirarua mavazi yake kama ishara ya majonzi. Lakini Mungu anasema:
“Rarueni mioyo yenu wala si mavazi yenu.” (Yoeli 2:13)
Hapa Mungu anasisitiza mambo matatu:
(i) Toba ya kweli ni ya ndani
Siyo machozi ya nje tu.
Siyo kufunga bila kubadilika.
Siyo kwenda kanisani bila kuacha dhambi.
Ni moyo uliovunjika mbele za Mungu.
(ii) Mungu anatazama moyo
Tunaweza kuwaficha watu, lakini hatuwezi kumficha Mungu.
Anaona kiburi, chuki, wivu, uasherati wa siri, dhambi za moyoni.
(iii) Mungu ni mwenye rehema
Yoeli anasema:
“Kwa maana yeye ni mwenye neema, rehema, si mwepesi wa hasira.”
Hii ndiyo tumaini letu katika Kwaresma – Mungu hatuiti ili atuangamize, bali ili atuokoe

*A. SHERIA – TUNAHITAJI KURARUA MIOYO YETU*

Je, mioyo yetu ikoje?
Je, tunaishi maisha ya mazoea tu ya kikristo?
Je, ibada imekuwa desturi tu?
Je, tunashika nafasi kanisani lakini mioyo iko mbali na Mungu?
Kwaresma ni wakati wa kujitazama:
Mahusiano yetu na Mungu yakoje?
Maisha ya maombi yakoje?
Tumeacha dhambi kweli au tunazificha?
Mungu anatuita: Rarua moyo wako.

*B. INJILI – MUNGU ANARUDISHA NA KUJESHA*

Yoeli 2:18–19 inaonyesha Mungu akihurumia watu wake.
Baada ya toba ya kweli:
Mungu aliahidi kurejesha mavuno.
Aliahidi kuondoa aibu.
Aliahidi kuwalinda dhidi ya adui.
Hii ni picha ya Kristo.
Katika Kwaresma tunamwangalia Yesu:
Anaenda Yerusalemu kwa ajili yetu.
Anakubali mateso kwa ajili ya dhambi zetu.
Anamwaga damu ili kutusafisha.
Tunaporarua mioyo yetu kwa toba, Kristo anatujaza rehema na msamaha.
Hakuna dhambi kubwa kuliko neema ya Mungu

*MWITO WA MAISHA MAPYA*

Yoeli anawaita watu wote – wazee, vijana, watoto.
Maana yake:
Hakuna aliye nje ya wito wa toba.
Hakuna aliye mkamilifu asiyohitaji neema.
Katika Kwaresma hii:
Rudisha ibada ya familia.
Ongeza muda wa maombi.
Samehe waliokukosea.
Acha dhambi inayokutesa.
Jitoe zaidi katika huduma.
Hiyo ndiyo “kurarua moyo.”

*MAANA YA JUMATANO YA MAJIVU*

Majivu ni ishara ya:
Unyenyekevu
Kukumbuka kwamba sisi ni mavumbi
Kutubu na kurejea kwa Mungu
Lakini kumbuka:
Majivu kwenye paji la uso hayasaidii kama moyo haujabadilika.
Mungu hataki alama ya nje tu.
Anataka moyo uliotubu.
*HITIMISHO*
Wapendwa,
Yoeli anatufundisha kuwa:
Toba ya kweli huanzia moyoni.
Mungu ni mwingi wa rehema.
Baada ya toba, kuna urejesho.
Leo, Mungu anakuita binafsi:
“Rarua moyo wako.”
Usingoje kesho.
Usingoje Pasaka.
Anza leo.
Kristo yuko tayari kukusamehe, kukuponya, na kukurejesha.

*SALA YA KUFUNGA*

Ee Mungu wetu mwenye rehema,
tuvunje mioyo yetu ya mawe, utupe mioyo mipya.
Tujalie toba ya kweli katika kipindi hiki cha Kwaresma.
Utusafishe kwa damu ya Yesu Kristo,
ili tuishi maisha mapya ya utakatifu na upendo.
Katika jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu.
Amina.
Ev.John
whatsapp:0768386606

KKKT DKU SIKU YA BWANA YA 7 KABLA YA PASAKA

*IBADA YA TAREHE 15 FEBRUARI 2026*
SIKU YA BWANA YA 7 KABLA YA PASAKA (QUINQUAGESIMA/ESTOMIHI)

*YESU AIENDEA NJIA YA MATESO YERUSALEMU*
ZABURI 48:1-8; RUMI 11:25-27

*SOMO LA MAHUBIRI: MATHAYO 17:22-23*
WIMBO: TMW 415
MAFAFANUZI

1. *UTANGULIZI*
Katika Injili ya Mathayo Yesu anatabiri juu ya mateso, kifo na kufufuka kwake mara tatu. Hii inaonesha kuwa mateso na kifo cha Yesu hayakutokea kwa bahati mbaya bali yalikuwa sehemu kamili ya mpango wa Mungu wa wokovu. Utabiri huu unajitokeza katika Mathayo 16:21–23; 17:22–23; 20:17–19. 

Utakachokiona katika utabiri huo ni kwamba, hata kama alizungumza habari za kutiwa mikononi mwa wakuu wa makuhani, kuteswa na kuuawa, bado kila mara alimaliza na kufufuka kwake. Maneno mengine yaliweza kukosekana, kwa baadhi ya tabiri; lakini kila mara kufufuka kumejitokeza. Hii ina maana kwamba, hata kama mateso ilikuwa lazima, Yesu alikuwa anatazama mbele kwenye matokeo ya hayo yote. Hapuuzii uwepo wa mateso dhihaka na kifo, lakini anaona kwamba hayo yanatumika kumfikisha kwenye utukufu. Na katika kuyasema, hafichi. Anaweka wazi kuwa yatampata, Yeye mwenyewe, si mwingine. Mkazo huo ulikuwa wa muhimu ili kutimiza unabii wa Isaya 53  kuteswa kwa masihi (the Suffering Messiah). Na hii ina maana kubwa katika theologia. Kuwa mfuasi wa Yesu hakumwepushi mtu na mateso au changamoto, bali kuna mthibiitsha kuwa yeye ni nani hata anapkuwa katika mateso. Na uthibitisho hapo ni kwamba, mateso yajapokuwa makali kiasi gani, ushindi upo. 

Wanafunzi walipaswa kujifunza maana ya ufuasi lakini hilo lilifichwa machoni pao, aliwaambia mtu akitaka kunifuata ajikane nafsi yake auchukue msalaba wake (Mathayo 16:24). 

*Mathayo sura ya 17 in sehemu kuu tatu:* 
(a)  *Mathayo 17:1-13 Utukufu wa Yesu unaofunuliwa*
Mistari nane ya kwanza inahusu Yesu kugeuka sura (17:1-8). Yesu alionekana katika utukufu wa hali ya juu sana na sauti ya Baba ikathibitisha utambulisho huo. Hiki kilikuwa kilele cha ufunuo wa Yesu. Halafu yanafuata mafundisho kuhusu Eliya/Yohana Mbatizaji  (17:9-13). Yesu ni Mwana wa Mungu na utimilifu wa torati na manabii. Lakini hali halisi ni mateso. Yohana mbatizaji alikuja wakamtesa. Vivyo hivyo watamtenda Mwana wa Adamu. 

(b) *Mathayo 17:14-21 Udhaifu wa Wanafunzi na dai la Imani*
Waliposhuka bondeni wanafunzi waliendelea kushuhudia hali halisi ya dunia, kijana aliteswa na pepo na wanafunzi waliteswa na Imani ndogo. Kwa hiyo wale wanafunzi watatu waliorudi na Yesu toka mlimani walikutana na maumivu ya dunia ambayo walitamani kuyakimbia waliposema wajenge vibanda 3. 
Wanafunzi 9 waliobaki bondeni wakati Yesu ameenda mlimani na wanafunzi 3 walishindwa kutoa pepo. Ndipo Yesu akatoa fursa hiyo kufundisha kuwa Imani ni kama chembe ya haradali. Nguvu ya huduma haitoki kwa mwanadamu bali inatoka kwa Mungu kupitia Imani. 

(c)  *Mathayo* *17:22* – *27* Njia ya Msalaba na Maisha ya wanafunzi duniani

Sehemu hii inahusu utabiri wa Yesu juu ya kuteswa, kufa na kufufuka kwake. Halafu ilifuata habari ya kodi na uhuru wa mwana. Kwa hiyo utukufu wa Yesu unaelezwa kwa njia ya msalaba. Na msalaba ni alama ya unyenyekevu na mateso. Kazi ya yake  ni kumfanya mtu anyenyekee kwenye kila mfumo. Kwa watawala – mtu awe mnyenyekevu; katika kuutumia uhuru wake, asijiinue, napo pia awe mnyenyekevu. Kazi ya mateso na msalaba ni kumleta mtu kwenye ukuu wa kweli – yaani ukuu wenye unyenyekevu na uliojaa upendo.  

Mathayo 17:22-23 tunakutana na siri ya mpango wa Mungu juu ya wokovu na hiki ndicho kitovu cha sura ya 17. Baada ya kuona utukufu pale mlimani, mateso ya dunia, udhaifu wa imani ya wanafunzi, Yesu anafunua sababu ya yote hayo na suluhisho lake. Hii ni njia ya msalaba na ufufuo. Kung’aa kusingeeleweka na mateso ya dunia yangetupeleka kukata tamaa na kukosa matumaini .
Mathayo 17:24-27 ni aina ya maisha ya wanafunzi baada ya kujua siri hiyo kuu. Wanaishi kwa unyenyekevu, wanalipa kodi ili kutowakwaza wengine, wanatumia uhuru wao kwa kwa unyenyekevu unaotokeza upendo na uwajibikaji.
2. *MATHAYO* *17:22* – *23* *UTABIRI* *WA* *PILI*
Walipokusanyika (walipokaa) Galilaya Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba Mwana wa Adamu anakwenda kutiwa katika mikono ya watu, nao watamwua na siku ya tatu atafufuka. Wakasikitika sana. Hili si tangazo la kawaida, wala si tangazo la hofu na kushindwa bali ni taarifa ya mpango wa kazi ulioko mbele yao. Wao walikuwa hawaoni, kwa hiyo anawaambia mapema: msishituke, mpango unaofuata ni huu. Taarifa hii ilikuwa inawaandaa kisaikolojia. Na Kitheologia tunasema, ikiwa mtu anazunguka huko na huko akisema habari ya kifo chake na kufufuka kwake hata kabla havijatokea, ama ni kichaa au ni Mwana wa Mungu. Na kwa habari ya Yesu, alikuwa anawaambia jambo ambalo walikuwa hawajui. Hata kama mimi nipo katika mwili, ”Mwana wa Adamu”, mimi nina asili ya uungu. Hasemi kwa maneno, lakini maana ya kazi na ratiba anayoonesha inaibua hayo.

*Mwana wa Adamu*
Kwa mara ya kwanza habari ya Mwana wa Adamu inaonekana katika Danieli 7:13-14. Danieli anaona maono ya mbinguni, ambako kuna viumbe wa rohoni. Hata hivyo, kuna jambo la peke, anamwona mtu mwenye mwonekanekano au mfano wa mwanadamu – ndio maana ya Mwana wa Adamu. Danieli haelezi kirefu. Lakini alichokiona kimekuja kuwa wazi katika Yesu Kristo. Mungu ameuchukua mwili na kwa huo anatumia kuwakomboa wanadamu. Kwa huo atakuwa miongoni mwa watu – Mungu pamoja nasi; kwa huo atateswa. Alishuka na kunyenyekea lakini kunyenyekea kwake kumekuwa sababu ya wokovu kwa ulimwengu. Maana kama angebaki katika roho, hakuna mtu angethubutu kuunyosha mkono wake na kumtesa. Na hii ndio siri ya Kimasihi, na hapa neno Mwana wa Adamu limekuwa jina linaloficha siri kuu. Kuielewa unahitaji utulivu. Anajiita Mwana wa Adamu makusudi – anaficha asili yake halisi.

*Mwana wa Adamu anakwenda,* hili linaonesha kuwa ni safari ya makusudi kuuendea msalaba. Mungu katika mwili (Mwana wa Adamu) anakwenda msalabani. Kwa asili mwanadamu hukimbia hatari lakini Yesu anakaza uso kuyaendea mateso. Anayaendea mateso kwa upendo mkubwa wa kujitoa kwa sababu anajua nini anachofanya. Amekuja Kutenda mapenzi ya Baba, anajitoa kwa ajili ya rafiki zake ambao wana dhambi sio watakatifu. Yohana 15:13 Hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake. Asingeweza kuyafanya hayo kama asingekuwa Mungu. Na sisi hatuwezi kujitoa kwa ajili ya wengine, Mungu asipokuwa ndani yetu. Hatuwezi kama ndani yetu hakuna Kristo.
*Anakwenda kutiwa au kukabidhiwa* (Kiyunani – paradidosthai). Anakaribia kukabidhiwa mikononi mwa wanadamu. Si tu kwamba atasilitiwa bali anakabidhiwa kwa makusudi yaliyomo katika mpango wa Mungu. Ni mpango wa Mungu unaotendeka kupitia mikono ya waovu. Yesu hasukumwi na mwanadamu bali anakabidhiwa kulingana na mpango wa Mungu wa wokovu (Isaya 53; Mdo 2:23). Ndio maana hili halikuweza kutendeka hadi wakati wa Mungu ulipotimia.
*Watamwua:* Hii inasisitiza kuwa tukio hilo ni la uhakika sio uwezekano. Hata kama Petro alijitahidi kusema, Hasha, hilo halikupati wewe alikuwa anapingana na mpango wa Mungu ambao ulikuwa lazima kwa vile hapakuwa na njia nyingine ya kuleta wokovu isipokuwa kupitia kifo cha Yesu, ndio maana alimwambia nenda nyuma yangu Shetani.
*Siku ya tatu atafufuka:* Mungu Baba ndiye aliyemfufua. Kufa na kufufuka kwa Yesu ndio msingi wa Imani yetu. Hata Kiri zetu za Imani ya Mitume na Nikea zinasimama katika Imani hiyo ya kwamba aliteswa, akafa na siku ya tatu alifufuka kutoka kwa wafu. Hata mahubiri ya Petro (Mdo 2; 3; 4) yalijengwa katika Habari za kufa na kufufuka kwa Yesu. Mtume Paulo katika 1 Korintho 15:3-4 kwamba alikufa na kufufa kama yaneyavyo maandiko (15:14) anaonesha kuwa bila kufa na kufufuka kwa Yesu, Imani yetu ni bure. Je, kanisa la leo mkazo wa mafundisho yake upo wapi? Ikiwa tutaacha kusisitiza haya, ni wazi kwamba tunajenga kwenye msingi usio sahihi.
*Wanafunzi wakasikitika sana au kupita kiasi:* Hawakuelewa ufufuo hadi Yesu alipokufa na kufufuka ndipo macho yao yalifumbuliwa. Walikuwa na uhusiano wa karibu na Yesu na wasijue hatima yake.

3. *YESU AIENDEA NJIA YA MATESO YERUSALEMU.*
Hii ni jumapili ya mwisho kabla ya majira ya Kwaresma (Quinquagesima). Kanisa linaanza kuelekeza macho toka utukufu Kwenda msalabani. Kutoka miujiza Kwenda mateso yaletayo ukombozi wa kudumu, wokovu kamili katika kifo na ufufuo wa Yesu. Jumapili hii ya mwisho ni lango la kuingia majira ya Kwaresma. Ni majira ya kuacha kutazama miujiza na kuanza kutazama msalaba. Ni wakati wa kutangaza kuwa injili ya wokovu ni ya neema katika Yesu Kristo kwa njia ya Imani. Kwa hiyo taarifa ya safari ya Yesu sio ya huzuni bali injili ya neema inaanza kufunguka na kujidhihirisha, tunaelekea utukufu wa juu kabisa wa Yesu. Lakini Yesu alitamka jambo ambalo wanafunzi hawakutaka kulisikia kabisa. Yesu anaenda kufa Yerusalemu! Mfalme au Masihi aende kufa.

Ndio hii ndio habari njema, Yesu anaenda mwenyewe, hakukimbia wala kujificha . Huu ndio upendo wa kweli. Alilipa gharama ya wokovu wetu kwa njia ya kifo chake msalabani. Hii inatukumbusha kuwa dhambi ni mbaya sana, hukumu ya Mungu ni ya kweli, lakini neema za Mungu ni kuu zaidi. Yesu anauendea msalaba sio kwamba hakuwa na hofu bali aliishinda hofu bali alikuwa anatii mapenzi ya Mungu, alijua thamani ya safari yake, kumwaga damu ili kumwokoa mwanadamu ambaye alimkosea Mungu akawa hana njia ya kujiosha mwenyewe, alihitaji neema, kulipiwa gharama.

Siku ya tatu atafufuka, tunasikia sauti ya pasaka ndani ya tangazo la kifo. Mateso sio mwisho wala kifo sio mwisho wa ushindi wa Yesu. Hii inatukumbusha sisi kuwa siku ya tatu ipo, huenda tunapitia mateso, maumivu, kukata tamaa Mungu ana siku ya tatu kwa ajili yetu.
Wanafunzi walisikitika kupita kiasi, waliona kama ni mwisho wa ufuasi wao walioutaabikia miaka 3, waliona msalaba bila ufufuo, hata kama walikuwa wamesikia akiusema. Kumbe kuna wakati tunaweza kusikia jambo, lakini tusielewa kabisa lina maanisha nini. Na mara nyingi tunakutana na mambo na hatuyaelewi yanamaanisha nini.

Tunapoingia majira ya Kwaresma tuutazame msalaba kama daraja la kutuvushia kwenye utukufu. Na kwa sababu peke yetu hatuwezi kuvuka, majira ya Kwaresma yanatuita kwenye unyenyekevu na toba. Ni majira yanayotuambia kuwa tuache dhambi ili tuupokee wokovu. Macho yetu yasibakie kwenye vitu tulivyo navyo sasa, bali yatazame kwenye matokeo ya utii ulioanzishwa na Yesu, na kisha ukaja kwetu. Kwaresma inatukumbusha kuwa Yesu alitii mapenzi ya Baba akawa sababu ya wokovu kwa wale watakaotii mapenzi ya Baba. Kipindi hiki cha Kwaresma kinatukomaza zaidi katika kutembea njia ya utii. Basi na tutembee pamoja na Yesu kwenye njia ya utii – kuna kusalitiwa (tena na watu wetu wa karibu), kuna kuteswa, na kuna kuuawa; lakini huo sio mwisho wa habari. Baada ya hayo yote, kuna utukufu na huo ndio utukufu wa kweli. Tukielekeza macho yetu kwenye utukufu huo, mapito na mateso ya wakati huu hayatatuzui kwa lolote. Mungu atujalie kutembea kwa ujasiri katika njia ya msalaba ambao Yesu anauendea.
Amen.

IBADA YA TAREHE 06 AGOSTI 2023 SIKU YA BWANA YA 9 BAADA YA UTATU

Somo:TUENENDE KWA HEKIMA
ZABURI 119:161–168; MATHAYO 10:5–15, MITHALI 1:1–7*
WIMBO: TMW 294
MAFAFANUZI
1. UTANGULIZI: Mithali 1:1
Kitabu kinaitwa Mithali za Sulemani, mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli. Kitabu hiki ni mkusanyiko wa misemo ya hekima kuhusu hali halisi ya maisha ya kila siku yenye busara na haki ikigusa mada mbali mbali. Kitabu kinatoa mafundisho yenye mafumbo ambayo yalikuwa ya kawaida katika Maisha yao ya wakati ule. Ni misemo mifupi mifupi ambayo ni rahisi hata kuikariri. Kama vile Mfalme Daudi alivyo chimbuko la Zaburi katika Israeli ndivyo Mfalme Sulemani alivyo chimbuko la hekima katika Israeli. Inatajwa kuwa Sulemani aliandika Mithali 3,000 na nyimbo 1,005 wakati wa maisha yake (1 Wafalme 4:32–34). Na wakaenda Mataifa yote kwa Sulemani ili waisikie hekima yake.

Kitabu hiki kinaitwa Mithali za Mfalme Sulemani wa Israeli, lakini ni hakika kwamba Sulemani hakuziandika zote. Nyingine zinatajwa kuwa ziliandikwa na Aguri bin Yake (Mithali 30:1–33) na Mfalme Lemueli (Mithali 31:1–9), na wengine wametajwa kuwa wenye hekima bila kutajwa majina yao (Mithali 22:17 na 24:23). Mkazo ni kufundisha hekima ya jinsi ya kuishi maisha yanayompendeza Mungu. Sura nne za kwanza ni mkazo juu ya asili ya hekima na umuhimu wake na sura zinazofuata ni mkusanyiko wa mistari miwili miwili mifupi yenye mithali zenye nguvu zinazogusa mambo mbali mbali ya maisha kama ndoa, upendo, uvivu, bidii ya kazi, maonyo kuhusu ulevi na uasherati.

Mfalme Sulemani alifahamika kwa umaarufu na upekee wa hekima ya ajabu. Sulemani alipopewa nafasi na Mungu katika ndoto ya kuomba jambo lolote atakalo, aliomba hekima ya kuliongoza taifa la Israeli na Mungu alijibu ombi lake (1 Wafalme 3:3–13). Zipo habari katika kitabu cha Wafalme wa kwanza zinazoonyesha jinsi alivyotumia hekima aliyopewa na Mungu. Mfano maarufu ni wa kesi ya wanawake wawili makahaba ambao walimgombania mtoto aliye hai wakimkataa aliye kufa (1 Wafalme 3:16–28).

2. MITHALI 1:2-7 KUSUDI KUU LA KITABU
Mwanzoni kabisa mwa kitabu Sulemani anaelezea kusudi la kitabu cha Mithali. Ni kujenga maisha ya uadilifu yanayofaa kimwili na kiroho. Kumpatia msomaji hekima, busara na maarifa ya Kimungu. Yanatajwa makusudi makuu matatu:

(a) Ili kuwapa wajinga werevu (Mithali 1:4).
Kuwapa wajinga, au watu wa kawaida werevu au busara. Hao ni watu wasio wasomi, hawa ndio wenye kiu ya kupokea mafundisho. Kitabu hiki kinapaswa kuwafundisha hawa wasio na uzoefu ili kujua nini cha kufanya na wafanye namna gani katika maisha yao. Na kijana atapata utambuzi au ufahamu hata kwa mambo ambayo hakuyafahamu. Sifa moja wapo kubwa ya watu wa kawaida (simple people) au ambao wametajwa kuwa wajinga ni wepesi. Mithali 14:15 inasema: Mjinga huamini kila neno, bali mwenye busara huangalia sana aendavyo. Huyu mtu ni mwepesi au hata inaweza kusemwa kuwa ni mjinga, anaweza kuwa na maoni lakini akakosa hoja za nguvu.

(b) Kuwapa vijana maarifa na tahadhari (Mithali 1:4)
Vijana na wale watu wepesi wapo kuelekea utu uzima au kwenye hekima. Kitakachowapa tahadhari na uchaguzi sahihi katika maisha haya ni kukubali kufundishwa hekima. Hata nyakati za sasa kuna mambo mengi yanahitaji kuchambua kwa hekima na kuishi maisha ya tahadhari. Nyenzo ya kuishi maisha ya tahadhari ni hekima.

(c) Kuwaongezea elimu wenye hekima na mwenye ufahamu ayafikie mashauri yenye njia (Mithali 1:5-6) waweze kuishi maisha ya uadilifu.

Kumbe kitabu cha mithali hakipo kwa ajili ya wajinga na wale wasio na uzoefu tu bali hata kwa wale wenye hekima. Kwa kupitia mafundisho ya mithali hizi wenye hekima wataongezewa elimu zaidi na zaidi. Mwenye ufahamu atafikia mashauri yenye njia, yanayomwezesha kutatua matatizo magumu kama ilivyokuwa na mfalme Sulemani alipoletewa kesi ya wale wanawake wawili waliogombania mtoto. Kumbe hakuna mwisho katika kutafuta maarifa na hekima.
Anasema mithali zinampelekea mtu kujua hekima na adabu, kutambua maneno ya ufahamu na kufundishwa matendo ya busara katika haki na hukumu na adili. Katika kujua hekima ifahamike kwa kizazi chetu kinaitwa cha habari na upeanaji wake (information age) lakini sio wengi katika kizazi hiki wanaotafuta hekima. Kujua maneno ya ufahamu maana yake yameandikwa yanapaswa kusomwa au kuangaliwa. Mithali 3:21 anasema Mwanangu, yasiondoke haya machoni pako, shika hekima kamili na busara.
Kujua hekima: Kuna tofauti kati ya hekima (wisdom) na maarifa (knowledge). Mtu anaweza kuwa na maarifa au ufahamu lakini asiwe na hekima. Kwani maarifa (knowledge) ni mkusanyiko wa ukweli wa mambo (facts about things) lakini hekima (wisdom) ni matumizi sahihi ya vile ambavyo tunavifahamu katika maisha yetu. Maarifa au ufahamu (knowledge) yanaweza kutuelezea namna mfumo wa utawala wa fedha lakini hekima ndiyo itasimamia matumizi sahihi ya fedha, kwa mfano kusimamia makisio ni hekima zaidi kuliko utaalamu. Shida yetu leo watu wengi wamejikuta wanatafuta fedha na sio hekima. Wengi tunaweka nguvu katika kupata elimu na sio hekima. Swali linakuja, hekima inatafutwaje? Mithali 1:7 na Zaburi 111:10 zinaweka wazi kuwa kumcha Bwana ndio mwanzo wa hekima. Kumbe hekima na maarifa vyanzo vyake ni kumcha Bwana. Na ukienda kwa Ayubu 28 unaona maelezo marefu kabisa.
Kufundishwa matendo ya busara/hekima
Mithali zipo kama shule au chuo cha hekima. Lakini tuingie chuoni tukiwa na moyo pamoja na akili wazi kupokea mafunzo. Tukifanya hivi haki, hukumu na adili/usawa vitatokea katika maisha yetu.

Lakini msingi mkuu wa hekima na maarifa ni kumcha Bwana ambacho ndicho chanzo cha maarifa yote (Mithali 1:7; Zaburi 111:10). Kitabu cha mithali kimeweka mkazo wake katika mambo halisi ya maisha na sio nadharia. Lakini kinatupa ukweli kwamba msingi ni fundisho la kitheologia kuwa maarifa na hekima yanatokana na kumcha Mungu, kuwa na hofu ya Mungu. Hofu ya Mungu ni kumjua Mungu, kujitoa kwa Mungu, kujinyenyekesha kwa Mungu.

3. TUENENDE KWA HEKIMA
Wiki iliyopita tuliongozwa na kichwa kinachosema uchaguzi wa busara na leo tunazunguzia hekima. Mara nyingi tunajikuta tunatumia maneno haya mawili kwa wakati mmoja, hekima na busara. Nimeeleza kwa kirefu tofauti zake katika kitabu cha Mafafanuzi ya Mahubiri ya mwaka 2020 ukurasa wa 199 na ukurasa wa 205. Kwa haraka utaona kuwa hekima ni pana kuliko busara. Hekima inasimama kama usukani wa kuendesha busara.

Somo letu linatuhimiza kuenenda kwa hekima katika dunia ambayo imebadilika mno katika mfumo wake. Mahusiano katika ndoa yameingia changamoto kubwa mno. Migogoro katika ndoa ni mingi. Ukiangalia kwa undani utagundua kuwa kuna vitu vya msingi vinakosekana. Maarifa ya maisha ya ndoa na hekima za Kimungu zimekosekana. Na mahali fulani imeelezwa kuwa ndoa za watu walioenda shule ndio zinaongoza kuleta shida, kumbe maarifa na elimu vimeshindwa kuleta maelewano katika ndoa. Biblia imeshatuambia chanzo cha maarifa na hekima ni kumcha Bwana. Mungu asipopewa nafasi halisi katika maisha yetu hakuna usalama.

Hata wale wanaoonekana kama wacha Mungu, watu wa dini sana wamepata shida hiyo hiyo kwa sababu ya kukosekana kwa misingi ya kweli ya neno la Mungu. Akili zimeshindwa kufundishika. Neno linasema: Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea, nitakushauri jicho langu likikutazama (Zaburi 32:8). Mfano wa ndoa ni mmoja tu. Zipo changamoto nyingi zaidi ya hizo ambazo zinahitaji hekima za Mungu.

Kuna hitaji hekima katika malezi ya watoto na mahusiano kati ya wazazi na watoto, katika kutunza mazingira yetu, katika kutafuta na kutumia fedha.

Mambo yote haya kwa kutumia maarifa yetu hatuwezi kuyamudu, maana adui yupo kazini wakati wote. Tunahitaji uongozi wa Mungu. Na uzuri wake ni kwamba, ndani yetu huishi Roho wa Mungu. Huyu ndiye hekima yetu na mwongozo wetu kwa kila jambo. Maana yake, ili kuenenda kwetu kuwe kwa hekima, lazima tuhakikishe tupo na yeye aliye asili ya hekima. Mungu atusaidie tumpe nafasi Roho wake maana ni katika yeye tutakuwa na hekima na hivyo tutaweza kuenenda kwa hekima. Amen.

IBADA YA TAREHE 30 JULAI 2023 SIKU YA BWANA YA 8 BAADA YA UTATU

Somo:WEMA WA MUNGU WATUVUTA TUPATE KUTUBU
ZABURI 27:5-10; 2 KOR. 7:7-12;HOSEA 14:1-3*
WIMBO: TMW 149
MAFAFANUZI

1. UTANGULIZI

Ujumbe wa kitabu cha Nabii Hosea uliwasilishwa kwa njia ya kuigizwa katika Maisha ya nabii mwenyewe. Kwa mtazamo wa utumishi na ufuasi haikuwa njia rahisi ya kuwasilisha ujumbe. Nabii Hosea aliagizwa na Mungu kuoa mwanamke kahaba na kuzaa naye watoto. Mungu alisema anafanya hivyo kwa sababu nchi imefanya uzinzi mwingi. Mwanamke aliyemwoa aliitwa Gomeri (Hosea 1:2-3). Hata baada ya kuolewa na Nabii Hosea, Gomeri aliendelea kwenda kufanya uzinzi na wanaume wengine na Hosea aliendelea kumrudisha na hata kumnunua kwa fedha ( Hosea 3:2).

Katika mlango wa tatu nabii anafafanua alichoagizwa na Mungu kufanya na sababu za kufanya hivyo. Aliagizwa ampende mwanamke apendwaye na Rafiki yake naye ni mzinzi, kama vile Mungu awapendavyo wana wa Israel ingawa wamegeukia miungu mingine (Hosea 3:1).

Ndani ya ujumbe wa Hosea kuna onyo kwamba kama Israeli hataacha uzinzi (kuabudu miungu mingine) ataadhibiwa vikali. Lakini kumbuka, adhabu huwa na lengo la kumrekebisha mkosaji. Hukumu ndio shida. Labda mhukumu awe na huruma. Sura zinazofuata Hosea 4-13 zinahusu Mungu na Israeli asiye mwaminifu. Ndani yake sura za 4 na 5 zinazungumzia uzinzi ambao Israeli anaufanya kwa kuabudu miungu mingine. Sura ya 6 Efraimu alirudi kuadhibiwa. Njooni tumrudie Mungu maana yeye amerarua na yeye atatuponya (Hosea 6:1); Sura za 7-12 Israeli (Efraimu) atapona hukumu kama atamrudia Mungu anayempenda. Efraim ni kabila ambako wafalme wengi walitoka. Sura ya 13 Israeli atahukumiwa sasa na sura ya 14 inaonyesha kuwa Israeli ataokolewa baadaye.

Ukijumlisha ujumbe wa Hosea unakuwa tabia yao ya kutokuwa waaminifu ndio sababu ya hukumu itakayokuja. Hii sura ya mwisho ni ya matumaini kwa taifa lililotubu. Hosea aliitwa kuhudumu katika taifa lililochanganyikiwa na limepoteza maadili na uchaji. Alipewa wajibu mkubwa mno wa kuoa kahaba na yeye kubaki mwaminifu katika ndoa yake kama Mungu alivyo hata kama mke wake alikwenda kwa wanaume wengine.

Fikiria tu njia hii ya kuwasilisha uasi ambao umefanywa na wana wa Israeli angepewa mchungaji mmojawapo leo. Kwanza, yeye mwenyewe angesema hiyo sio sauti ya Mungu na wale wanaoogonzwa naye wengi wangetia mashaka kama kweli ni Mungu ameruhusu hilo.

2. HOSEA 14:1-3

Sura hii ya mwisho ya kitabu cha Hosea inakuja na kitu cha pekee baada ya kutupitisha kwenye ujumbe wa hukumu. Anakuja na ujumbe wa rehema. Rehema ni msaada unaoambatana na huruma. Mungu mwenyewe anatoa maelekezo namna ya kufanya toba ili kumrudia Mungu. Anaelekeza ili kufikia toba nini cha kusema na nini cha kufanya. Ujasiri wa kutubu unajengwa na utayari wa Mungu kuwapokea wenye dhambi wanaporudi. Mungu anasema nitawaponya kurudi nyuma kwao, nitawapenda kwa ukunjufu wa moyo kwa maana hasira yangu imemwacha (Hosea 14:4,8). Pia zipo faraja kubwa ambazo ameziandaa kwa ajili ya Israeli anayetubu (Hosea 14:5,7). Ujumbe unahitimishwa kwa swali kwamba ni nani aliye na hekima na atayafahamu mambo haya? Na nani mwenye busara atakaye yajua? Ni maswali yanayotuhusu sisi sote katika ukweli wa kuyapokea haya (Hosea 14:9).

Hosea 14:1 Israeli mwenye dhambi anaitwa kurudi (kutubu).

Kumbe kila mtu anahitaji ujumbe wa toba hata walio ndani ya agano kama Israeli. Kwa hiyo hata Wakristo ndani ya kanisa wanahitaji ujumbe wa toba kila siku. Israeli mrudie Mungu wako kwa maana umeanguka kwa sababu ya uovu wako. Na kurudi ni kurejesha uhusiano (fellowship) uliopotea au uliovunjika. Ulipotea au kuvunjika namna gani? Ni pale walipoanguka au kujikwaa kwa sababu ya kuabudu miungu mingine na kumwacha Mungu aliye hai ambaye anawapenda. Ndio picha ya ndoa ya Hosea na Gomeri. Wanarudi kwa njia gani? Ni kwa kutubu na kutengeneza.

Hosea 14:2 Chukueni maneno pamoja nanyi

Wanaporudi wameelekezwa maneno ya kwenda nayo ambayo ni kumwambia Bwana: Ondoa maovu yote, uyatakabali yaliyo mema. Na hivyo ndivyo mtakavyotoa sadaka za midomo yetu kana kwamba ni ng’ombe.
Wanapomrudia Bwana hawaendi kimya kimya na lazima waende kama Bwana anavyotaka na anavyoelekeza. Hataki wafikiri tu mioyoni na kujisikia hatia ya dhambi bali wakiri maneno hayo kwa midomo yao. Wamwambie Mungu kwamba tunakupenda na kwamba tumekukosea. Hata katika mahusiano yetu mfano ya mume na mke huwa ina nguvu kumwambia mwenzi kwamba unampenda, hata kwenye viapo vya ndoa wenzi huwa wanakiri kwa midomo yao kueleza upendo wao na kujitoa kwao katika ndoa. Katika viapo hivyo tunabeba maneno pamoja nasi. Mtume Paulo katika Warumi 10:8-10 anasema mtu kwa moyo huamini hata kupata haki na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu.

Je, tunachukua maneno gani pamoja nasi?

Hayo maneno sahihi ya kwenda nayo tunayapata kutoka kwa Mungu mwenyewe katika neno lake. Mfano Mdo 3:19 tunaambiwa tubuni basi mrejee, ili dhambi zenu zifutwe. Na Mathayo 3:2 Yohana alihubiri tubuni mwache dhambi zenu. Na Yesu alianza huduma yake kwa kuagiza toba, Mathayo 4:17 tubuni.. Upo umuhimu wa kukiri maasi yetu kwa midomo yetu. Zaburi 32:5 c; Nalisema nitayakiri maasi yangu kwa Bwana. Katika toba kuna umuhimu mkubwa wa mtu kukiri kosa alilofanya. Katika mifumo mingi ya kanisa wapo watu waliopewa wajibu wa kuwasikiliza wengine wanapotengeneza mambo yao na Mungu. Kuna wachungaji waliokula kiapo cha kufanya hivyo. Kuna watu wanafundisha kuwa inatosha kumwambia Mungu makosa yako, sawa lakini kuna mahali hali na hatia ya dhambi haiishi hadi mtu amekiri kwa midomo yake. Shida ni pale ambapo huduma imeingiliwa na watu ambao hawana dhamana ya kufanya hilo na kusimama kama mawakili wa siri za Mungu au wale wenye dhamana wanapokengeuka na kuharibu huduma. Lakini ukweli utabaki kuwa katika toba upo umuhimu wa kukiri kwa midomo yetu.

Tunamwambia nini Mungu katika toba yetu?

Ondoa maovu yote na utupokee kwa rehema zako. Hata katika sala ya Bwana Yesu alitufundisha kukiri makossa yetu mbele za Mungu ili atusamehe. Tunaporudi kwa Mungu lazima tunyenyekee mbele zake na kukubali kwamba tumekosa, tumefanya dhambi na tunahitaji msaada wake. Tunamhitaji yeye tu hatuna lolote la kufanya Zaidi ya kujiachia mikononi mwake.

Na ndivyo tutatoa sadaka ya midomo yetu kama sadaka ya ng’ombe. Maana yake maneno yetu ya toba na sifa mbele za Mungu ni sadaka ya kuteketezwa mbele za Mungu. Katika toba hiyo tutakiri wazi na kutengeneza mambo matatu:
(a) Kukataa kutegemea mataifa ya kigeni (Ashuru). Mungu pekee yake ndiye mwokozi wetu.
(b) Tutaacha kutegemea uwezo wa kivita kama kutegemea farasi (Zaburi 20:7).
(c) Tutakataa kutegemea sanamu, kazi za mikono yetu bali tutamtegemea Mungu pekee yake.
Wito wa nabii Hosea katika kifungu hiki (Hosea 14:1-3) ni kuwaita Israeli kurudi kwa Mungu kwa moyo wa dhati. Amewapa maneno ya kuomba wanaporejesha uhusiano wao na Mungu. Mwana mpotevu katika Luka 15:11-32 yeye alipanga maneno ya kusema anaporudi nyumbani kwa baba.
Kitabu cha Hosea kinahusu mambo ya dhambi na hukumu lakini pia upendo na huruma za Bwana kwa watu wasiostahili kama ambavyo Gomeri hakustahili kuwa mke wa nabii. Na Upendo huo wa Mungu umeonyeshwa kwa njia ya ndoa hiyo ya nabii Hosea na mwanamke Gomeri. Ni picha inayoumiza moyo kwa mtazamo wa kibinadamu, je, kwa Mungu mtakatifu sio zaidi?

3.WEMA WA MUNGU WATUVUTA TUPATE KUTUBU

Kutokana na mafunzo ya kitabu hiki utagundua kuwa kumbe Mungu anapomtendea mema huyu mwanadamu aliye mwovu sio kwamba anataka aendelee kutenda uovu bali anataka avutwe na upendo wa Mungu na hivyo aweze kugeuka na kujinyenyekesha kwa toba.
Mungu atujalie tutambue hilo na kutumia neema hiyo ya nguvu ya toba.
Amen.

KIPIMO CHA IMANI

Tangu nimeokoka nimebahatika kusikia mafundisho mengi sana mazuri kuhusu imani, wakati mwingine nilijifunza kuwa huhitaji imani kubwa kung’oa mlima, na nilipoijaribu imani ndogo kung’oa mlima, mlima uliishinda imani yangu ndogo. Je! Wapi hasa nilikosea mpaka kushindwa kuung’oa mlima mkubwa kwa imani ndogo? ( nadhani nilihitaji imani inayokua kama mbegu ya haladali, mpaka kuzidi ukubwa wa mlima ndipo niung’oe)

Leo ninataka kukueleza kipimo cha imani yako kwa maelezo haya.

Kama imani yako ya kufa ni kubwa kuliko ya kuishi basi jua huna imani au imani yako ni haba, hivyo kikubwa lazima kishinde kidogo.

Kama imani yako ya kutokupona ina nguvu kuliko kupona basi huna imani, au imani yako haba na chenye nguvu kitashinda.

Kama imani yako ya kukosa ni hakika kuliko ya kupata basi imani yako ni ndogo hivyo kukosa kutashinda, na kama imani yako ya laana ni zaidi ya baraka nakuhakikishia kila utakapoongea, utakachowaza, utakachoota, utakacokiona na kukikiri kitakuwa ni laana, balaa, mikosi na chenye nguvu kwenye akili yako, moyo wako na kinywa chako ndicho kitakachoshinda na kutokea kwenye maisha yako.

Nadhani umeshajipima kwenye eneo lako, sasa ni kazi yako kuhakikisha unaifanya imani yako iwe kubwa kuliko, mlima, magonjwa, madeni, na mahusiano ndipo utakapoweza kubadilisha mwonekano wa kinachokutisha kwa imani. KUMBUKA CHENYE NGUVU, UZITO, NA UHAKIKA NDICHO HUSHINDA.
Wakati wewe unaona haiwezekani kuna watu imewezekana, tofauti yako na yao ni kile unachokiona kigumu wao walikiona chepesi. Iga mwenendo wao utafanikiwa
Bwana akibariki sana.
#victoriousyear2020
contact 0768386606

IBADA YA TAREHE 23 JULAI 2023,SIKU YA BWANA YA 7 BAADA YA UTATU

Somo:UCHAGUZI WA BUSARA
ZABURI 37:1-8; LUKA 10:38-42
MATENDO 6:1-6*
WIMBO: TMW 422
MAFAFANUZI

1. UTANGULIZI
Hadi wakati huu wafuasi wa Yesu walikuwa wachache sana, lakini siku ya Pentekoste waliongezeka waumini elfu tatu (3,000). Kwa mujibu wa mwandishi wa Kitabu cha Matendo, Mungu aliongeza wanafunzi kila siku (Mdo 2:47). Mitume wakaweka nguvu zao katika kuhubiri, kufundisha, kuomba na kuombea wagonjwa (Mdo 3:1-26; 5:12-15), wakaongezeka wafuasi wengine elfu tano (Mdo 4:4). Kanisa la mwanzo lilikuwa vizuri sana katika kutunza takwimu hadi lilijua watu wangapi wameokoka, na lini.
Kanisa lilifanya mambo yote kuwa shirika. Likatunza wajane na wahitaji wengine (diakonia). Kwa vile mitume waliweka kipaumbele na mkazo wao katika kuhubiri na kuomba, suala la usimamizi wa mambo ya huduma (diakonia ). Walitambua kuwa kipaumbele ni neno na maombi lakini suala la diakonia bado lilionekana kuwa muhimu. Ndio maana kulipojitokeza manung’uniko kanisa lilichukua hatua haraka sana kwani lilijiona kuwa lilipaswa kufuata mfano wa Yesu wa kuwahudumia wahitaji, lakini pia lilifahamu kuwa hisia za ubaguzi ni hatari zinaweza kuligawa kanisa.
2.WATUMISHI SABA WAWEKWA KUJIBU MANUNG’UNIKO YA KUNDI LA WAYAHUDI WA KIYUNANI (MDO 6:1-7)
Kifungu kinachotangulia somo letu na kinachomalizia mlango wa tano (Mdo 5:42) kinasema: Na kila siku ndani ya hekalu na nyumbani mwao, hawakuacha kufundisha na kuhubiri habari njema ya Yesu kwamba ni Kristo. Na kutokana na kazi hiyo kanisa lilikua na kuongezeka kila siku. Na tatizo tunalokutana nalo katika somo letu linaashiria kwamba kasi ya ukuaji wa kanisa ilikuwa kubwa mno hadi wakashindwa kutawala mabadiliko hayo makubwa, wakashindwa kutoa huduma kwa watu kama inavyotakiwa. Kukatokea manung’uniko ya Wayahudi wa Kiyunani juu ya Waebrania kwamba wajane wao kwamba walisahauliwa katika huduma ya kila siku (daily service au Kiyunani kathemerinos diakonia).
Inaonekana kanisa lilikuwa limeweka mpango wa kuwasaidia wajane kupata mlo wa kila siku. Lakini kukatokea manung’uniko toka Wakristo ambao ni Wayahudi wa Kiyunani kwamba walisahauliwa kwenye mgawo wa chakula. Kwamba ni kweli au ilikuwa hisia tu hatujui. Kitu ambacho kinafahamika ni kwamba waliitisha mkutano wa jamii ya waaminio na kuwashirikisha changamoto hiyo na kutoa mapendekezo namna ya kulitatua. Kwa kuwa walikuwa wameweka vyote shirika (Mdo 4:34) inaonekana shida haikuwa kukosekana kwa chakula bali utaratibu wa kugawa. Lilikuwa suala la utawala na usimamizi.
Wale 12 wakaitisha mkutano na kushirikisha watu lile tatizo na pia wakaelekeza nini kifanyike. Hapa tunaona uamuzi wa busara kusikiliza tatizo na kulichukulia hatua mara moja. Wakagundua kuwa tatizo lile ni la utawala, wakasema, Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani (Mdo 6:2). Mitume walijua nini walikabidhiwa na Bwana Yesu (Mathayo 28:19-20; Mdo 1:8) walipewa wajibu wa kuhubiri na kufundisha neno na sio kugawa chakula au kufanya mambo ya utawala wa chakula. Haina maana kwamba kazi hiyo sio muhimu bali waliangalia vipaumbele vya wito wao na wajibu wa msingi.
Baadaye tunajifunza kuwa Kanisa lilifanya kazi kufuata vipawa mbali mbali ambavyo Mungu amevigawa ndani yake (Rumi 12:12-26; 1Kor. 12:27-31 na Efeso 4:11-16). Ni vema na ni muhimu kuheshimu vipawa ambavyo Mungu ametupa na kuwa waaminifu kwa wito wetu. Ingekuwa kosa kwa Mitume kuacha kuhubiri wakaanza kusimamia chakula. Mitume walijitambua kuwa hawakuitwa ili wawe kila kitu katika kanisa.
Mitume wakaelekeza kuwa basi chagueni watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili (Mdo 6:3). Wakataja sifa za hao wasimamizi au wadiakonia. Walitakiwa kushuhudiwa na watu kuwa na sifa ya wema, vinginevyo wasingeweza kuhudumu kwa ufanisi. Walipaswa kujawa na Roho Mtakatifu. Kazi yo yote kanisani inahitaji watu wenye Roho Mtakatifu na hekima za Mungu. Ushauri huu unafanana na ushauri ambao Yethro aliutoa kwa Musa (Kutoka 18:18-22). Kwa hiyo sifa hizo tatu za kushuhudiwa wema, kujawa Roho na hekima zinawahusu Makatibu wakuu, Watunza Hazina, watu wa utawala, madereva, makarani, nk. Mitume walisema watu wenye sifa hizo ndio wakabidhiwe jukumu hilo.
Mitume wakaeleza ni nini wao watajishughulisha. Wakasema sisi tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile neno (Mdo 6:4). Wanajibainisha kuwa kipaumbele kwao ilikuwa maombi na neno la Mungu. Kwa hiyo walitoa muda wa kutosha kwa ajili ya maombi na neno. Uchaguzi wa busara ni kujua vipaumbele na kuvitekeleza.
Neno hili likapendeza machoni pa mkutano wote (Mdo 6:5a). Hapa ni kwamba kanisa zima lilifurahi sio tu wale Wayahudi wa Kiyunani ambao walinung’unika. Wote walifurahi kupona kwa mwili wa Kristo ambao ulikuwa umejeruhiwa kwa sehemu mojawapo ya viungo kujeruhiwa. Hapakuwa na ushindani wowote hoja ilipokelewa na kutengenezewa suluhu ya pamoja.
Wakamchagua Stefano, mtu aliyejaa imani na Roho Mtakatifu, Filipo na Prokoro,na Nikanoni, na Timoni, na Permena na Nikolao mwongofu wa Antiokia (Mdo 6:5b). Hapa inaonekana Mitume hawakutaja mtu, waliacha mkutano wenyewe uchague watu. Na kwa kuangalia majina yote saba yana asili ya Kiyunani kwa hiyo ni kusema kama Wadiakonia wote walitoka upande wa wale walioonekana wajane wao kupunjwa. Hili inaonekana walilifanya kwa upendo kabisa. Kati ya hao Stefano ameelezewa kipekee na baada ya hapo tumesikia habari za Stefano mfia dini ila hatujasikia habari za wale waliobaki. Na kwa vile hatujasikia tena manung’uniko inawezekana kazi yao ya kusimamia utaratibu wa chakula ilifanikiwa vizuri.
Wakawaweka mbele ya Mitume (Mdo 6:6a). Baada ya wale watu saba kuchaguliwa ni kama waliwekwa mbele ya mitume ambao kwa wakati ule waliokuwa ndio mamlaka ya juu katika kanisa. Waliwekwa kama ili wawathibitishe. Hawa Mitume kama viongozi wa juu katika kanisa bado walikuwa wanafikika kwa urahisi ndio maana walielezwa tatizo lililo wakabili. Ni busara kufikika ili matatizo yawasilishwe mapema.
Mitume wakawaombea na kuwaweka mikono yao juu yao (Mdo 6:6b). Waliwekewa mikono ili kutumwa kwa kazi maalum (Mdo 13:3; 2 Timotheo 1:6). Waliwekewa mikono kuthibitisha uchaguzi ule na kuwatuma kazini. Hata nyakati za sasa katika kanisa watumishi wanawekewa mikono na kufanyiwa maombi wanapoingizwa katika kazi mbali mbali.
Neno la Mungu likaenea na hesabu ya wanafunzi ikazidi sana katika Yerusalemu, jamii kubwa ya makuhani wakaitii ile imani (Mdo 6:7). Kama Mitume walivyosema kwamba wao watadumu kuhudumu neno na katika maombi, matokeo yake kanisa likakua haraka sana pale Yerusalemu na makuhani ambao walikuwemo maeneo ya ibada ambapo Mitume walihubiri nao wakaamini na kutii imani. Kwa hiyo mahubiri na mafundisho ya mitume yaliwaongoa hata Makuhani.
3.UCHAGUZI WA BUSARA
Jambo kubwa katika somo letu limekuwa ni juu ya manung’uniko yaliyotokea katika kanisa la mwanzo. Kundi moja lilijisikia kubaguliwa. Kwa busara na kufikika kwa Mitume walifaulu kugundua kuwa hawapo salama kwa sababu kuna kundi linanung’unika. Leo kuna manung’uniko mengi katika jamii, katika familia, katika kanisa na katika nchi yetu. Inahitajika busara ya viongozi katika maeneo hayo kutopuuza na wachukue hatua ya haraka. Na mahali pengine manung’uniko yanatokea kutokana na hisia za kutotendewa haki au kubaguliwa. Ili kuondoa hisia wataalam wa sheria walisema, sio tu kwamba haki itendeke katika jamii bali ionekane kuwa inatendeka.
Katika kutafuta suluhu la tatizo lililolikabili kanisa la mwanzo tunakutana na uchaguzi wa busara ufuatao:
✓Kwanza, kusikiliza manung’uniko na kuyafanyia kazi hata kama hayana msingi ni jambo la busara.
✓Pili, katika kutatua tatizo mitume walishirikisha watu, huo ni uongozi shirikishi.
✓Tatu, Mitume walielekeza sifa za watu wa kuchaguliwa kuwa wawe wenye ushuhuda mzuri, waliojawa na Roho na wenye hekima.
✓Nne, Mitume waliacha watu wachague wenyewe na sio kuwashinikiza.
✓Tano, Mitume walifahamu vizuri mno wito wao na vipaumbele. Wakaweka nguvu zao katika maombi na neno. Kusimamia chakula na fedha sio kwamba hazikuwa kazi muhimu bali waliangalia vipaumbele na kugawana vipawa.
Katika mambo haya matano mara nyingi viongozi wengi nyakati zetu yamekuwa changamoto. Hawasikilizi manung’uniko hadi yanageuka kuwa migogoro, hata wakitaka kutatua wachache wanashirikisha watu na wanafanikiwa, wale wanaofanya bila kushirikisha watu hawafaulu. Jambo jingine la busara ni kuzingatia sifa za wale wanaopewa kufanya kazi ndani ya kanisa. Na suala la mwisho ni juu ya vipaumbele. Ni kiasi gani kazi zetu tunazifanya kufuata vipaumbele. Kwa mfano watumishi wengi wa madhabahuni tumepata shida kuweka katika uwiano shughuli za maendeleo na uchumi, fedha na mipango na suala la maombi na neno. Mungu atusaidie sana.
Amen.
Ev.john -0768386606

SIKU YA BWANA YA 13 BAADA YA UTATU

wazo la wiki: JIRANI YANGU

Masomo:
Zaburi 28:1-4
Mathayo 12:46-50
Matendo 28:7-10*
Rangi: KiJANI
Wimbo:TMW 410
UTANGULIZI
Leo tunatafakari juu ya mada ya Jirani zetu tukilitazama neno la Mungu kutoka
Matendo 28:7-10
> Jirani kulingana na tafsiri ya Kiswahili ni mtu yeyote aliye karibu na mahali
unapoishi.
> Jirani mi mtu muhimu sana katika maisha ya kila mtu, yawezekana anaweza kuwa
rafiki yako au adui zako.(Hekima inahitajika kuishi nae)
> Biblia tangu Agano la kale inaelekeza kuwa kila mtu anapaswa kumpenda jirani
yake kama nafsi yake( Law 19:17 – 18)
> Upendo wa namna hii haukuwa rahisi hivyo watu wengi walijitahidi kukwepa
wajibu huo na mara nyingi walihoji ni watu gani wanapaswa kuwa majirani.
Hata kipindi cha Yesu watu walijitahidi kumuuliza swali hili, na Yesu aliweka wazi
kuwa jirani ni :-
a. Mtu yeyote aliye na dhiki ni jirani yetu ( Lk 10: 29 – 37)
b. Jirani ni watu wote hata kama ni adui yetu ( Mt 5: 43 – 47)
Wajibu mkubwa aliopewa mwanadamu ni kumpenda Mungu na Jirani ( Mt 22:36-40,
Rum 13:8-10,Gal5:14,Yak2:8, 1 Yoh 4:20, Mt 3:28, 14:21)
Somo ambalo tumepewa kujifunza juu ya jirani kwa mwaka huu tunajifunza juu ya
jinsi ya kumtendea jirani hasa wale ambao tunafikiria hawawezi kuwa majirani.
1. AMRI IPO TUNAPOSHINDWA KUJITAWALA JUU YA JIRANI ZETU
> Mtu akifanyiwa ovu hupenda kulipa ovu kubwa zaidi na kuanzisha mashindano
baina ya watu waliogombana au kufanyiana maovu.
> Kutokana na kushindwa huku kujitawala hisia zao, kulisababisha haki kukosekana
katikati ya watu.(Law 24: 19 -20)
> Watu walipewa sheria ili iweze kusaidia ili adhabu iweze kulingana na Kosa.
2. WANA WA MUNGU WANAWAZA MEMA JUU YA JIRANI ZAO
> Kama nilivyoeleza kuwa jirani ni mtu yeyote mwenye dhiki hata kama akiwa adui
yako na unapaswa kumpenda kama nafsi yako
> Wajibu huu mzito wa kumpenda jirani kama nafsi yako uliendelea kuwatesa watu
wengi hadi kipindi cha Yesu.
> Kazi kubwa ya kukamilisha torati aliyoifanya Yesu katika mahubiri ya mlimani pia
aligusia suala la jinsi ya kukaa na watu kwa mtazamo mpya wa wana wa Mungu.
 Anawataka watu wa Mungu wasiwe na Mashindano juu ya uovu. Ukishindana
na uovu utajikuta inakuondolea uthamani wa kuwa mwana wa Mungu.
 Mtu akikufanyia jambo la kukuonea wewe usinung’unike fanya kwa upendo
utakaomshangaza mtesi wako; Jitahidi kuwa mkarimu kwake (Rum 12:20)
 Tusing’ang’ane kukariri neno la Mungu pasipo upendo wa kweli ndani yetu
kwa Mungu na jirani zetu
 Kuweka haja za wenzetu mbele kuliko matakwa yetu
 Tuwe na mizigo juu ya wengine (Mith 3:29)
3. MATENDO MEMA KWA JIRANI YANA MALIPO YAKE.
Jirani mtendee mema hata kama unaona hastahili, sababu unavyofanya hivyo sio
kwake tu bali unajitengenezea malipo yako Mbinguni na kujipa kibali cha kuwa
mwana wa Mungu ( Lk 6:35)
HITIMISHO
Mungu atuwezeshe tuweze kutambua thamani ya watu wengine zaidi kuliko makosa
wanayotutendea ili tuweze kuwatendea mema hata pale wanapotuudhi.
AMEN.
imeandaliwa na
Ev.John

MAHUBIRi Ya SIKU YA BWANA YA 12 BAADA YA UTATU

SOMO: TUTUMIE VYEMA NDIMI ZETU

masomo:
Zaburi 134
Mithali 10:11-13
Mathayo 8:1-4*

SHABAHA: WASIKILIZAJI WAELEWE YA KWAMBA KILA NENO LA ULIMI LAZIMA LITATOLEA HESABU KAMA JEMA AU BAYA SIKU YA HUKUMU

UTANGULIZI
Usemi ni uwezo mmojawapo wa mwanadamu wenye nguvu zaidi, kwa sababu kwa maneno yake anaweza kuleta manufaa makubwa, lakini pia anaweza kuleta hasara kubwa ( Mit 12:18,25; Yak 3:5,9)
Mtu awezaye kutawala ulimi wake anaweza kutawala nafsi yake yote ( Yak 3:1-4,7)
Uovu wa mtu huonekana kwa ulimi ambao haujatawaliwa ( Mk 7:21 – 23; Yak 3:6)
Maneno mengi ya mtu huonyesha upumbavu wake hivyo kila mmoja anapaswa kuutawala ulimi wake, utawala huo lazima uwe wa kweli isiwe ni kutumia maneno matamu tu ili afiche mawazo yake, yeye ni mnafiki na unafiki sio mzuri ( Zab 41: 5-6, Mit 10:18, Mt 22:15 – 18)
Ugeuzi wa maneno kwa ujanja au hila ni aina ya uongo ( Mit 12:19, 2Kor 4:2, Efe 4:25) Iwapo mtu anataka aseme ukweli kila wakati pia anatakiwa afanye hivyo kwa roho ya Upendo na maneno yake yaonyeshe tabia yake ( Mit 10:11, 20 – 21; 16:23; Efe 4:15, Yak 1:19)
Usemi wako unaonyesha hali yako ya kiroho na usemi huo utatumiwa siku ya hukumu kama ushahidi wako ( Mt 12: 36 – 37)
Hakuna neno ambalo Mungu halijui katika yale yote unayonena (Zab 139:4)

• Katika mistari hii miwili kutoka katika kitabu cha mithali inatufundisha mambo muhimu yafuatayo kuhusu matumizi ya Ulimi.

1. USEMI WA MWENYE HAKI UNA HEKIMA NA WEMA
Mtu aliye na hekima wakati wote anajua kuutunza ulimi wake, maneno yake wakati wote ni maneno yaliyokolea busara.
Maneno ya mtu wa haki yanatamani kuona mema kwa wengine na yamejaa hekima(Mith 10:20 – 21)
Mtu mwenye hekima si mwepesi wa kusema na akisema maneno yake yamejaa baraka na mema.

2. USEMI WA MTU MWOVU WAKATI WOTE UNADANGANYA NA KUUMIZA(Zab 10:7)
Mtu mwovu wakati wote huwaza mabaya kwa wengine na hupenda kutamka laana kwa watu wengine(Zab 52: 2 – 4)
Maneno yake yamejaa uongo na kujipendekeza( baadhi ya vitu asivyopenda Mungu Mith 6:17)
Mtu mwovu huwa mnafiki na kutaka kujionyesha kuwa ni mwema mbele za watu tu.

3. ULIMI MWOVU UTAADHIBIWA
Mungu atamharibu na kumuondolea mbali mwenye maneno mbaya ( Mith 10:31)
Atakuondoa katika nyumba yako( Zab 52:5)
Kifo kitampata mwenye ulimi wenye hila (Mith 17:20)

HITIMISHO
Mungu atusaidie tuweze kutumia ulimi wetu vizuri tukijua kuwa maneno yetu ipo siku tutayatolea hesabu.
AMEN.
imeandaliwa na mwinjilist John
KKKT -SD Njombe

#0768386606

JUMAPILI YA 11 BAADA YA UTATU 23/08/2020

Somo:TUWE WANYENYEKEVU
fungu;LUKA 21:28-33

Bwana Yesu asifiwe…..

Unyenyekevu ni nini? Unyenyekevu ni hali ya moyo na akili inayomfanya mtu ajikubali alivyo na awakubali wengine walivyo. Kwa njia ya unyenyekevu mtu anatambua analopaswa kutenda na analitenda na pia asilopaswa kulitenda na halitendi. Kwa njia ya unyenyekevu, mtu anawapa wengine nafasi ya kuwa wanavyotakiwa kuwa katika haki. Kwa njia ya unyenyekevu, tunakomesha vilema vyetu vyote vya majivuno, kiburi, maringo, kujionaona na kujikweza.

Fadhila ya unyenyekevu inachukuliwa kuwa ya msingi na kiongozi wa fadhila nyingine zote. Martin luther anaendelea kusema kuwa “Kimsingi ni katika unyenyekevu mtu anafanywa kuwa mfuasi wa Kristo, na kwa hilo roho inaandaliwa kuungana na Mungu.” Mambo yote ni lazima yapate msingi wake katika unyenyekevu. Unyenyekevu unachukua nafasi ya kwanza kwa vile, unafukuza majivuno.

Fadhila ya unyenyekevu inatudai kujishusha ili tuinuliwe. Inatufanya tujione si kitu ili tuonekane kuwa ni kitu. Inatufanya tuwajali zaidi watu kuliko kujijali na kujipendelea sisi wenyewe. Inatufanya tuoneshe upendo wetu zaidi kuliko kutaka kupendwa. Inatufanya tuwaheshimu zaidi wenzetu kuliko kutaka kuheshimiwa.

Kwa njia ya unyenyekevu, tunaweza kufundishwa, kuelekezwa, kuongozwa, kuonywa, kulindwa, kutetewa na kukuzwa kwa ujumla. Ni fadhila ya msingi sana katika maisha ya mahusiano ya kila siku katika familia na katika jumuiya yoyote ile ya watu. Hata marafiki wa kawaida tu, au wachumba wakikosa unyenyekevu basi mahusiano yao daima hayatakosa malumbano, matusi, dharau, ukandamizaji na kila aina ya mateso.

Pengine watu wengi hushindwa kuishi na sisi kwa sababu tunakosa unyenyekevu, na ndio maana, hatuonyeki, haturekebishiki hatupendeki, hatuelekezeki, hatufundishiki, daima tunajiona kuwa ndio wenye haki sana mbele za watu na mbele za Mungu. Kukosa unyenyekevu kunatutenga na fadhila za Mungu. Tazama yule mfarisayo aliyekosa unyenyekevu akajiona kuwa yeye ndiye mwenye haki sana. [Lk 18:9-14]

Familia isiyojua unyenyekevu, ni uwanja wa vita daima. Vita za maneno na za mikono hazitakwisha. Tangu mwanzo wa malezi watoto wafundishwe juu ya umuhimu wa unyenyekevu. Unyenyekevu ni tendo la kijasiri kwa sababu linakudai kujishusha, kukomesha maringo, kiburi, kujikweza na majivuno. Walio wanyenyekevu daima hupata kibali machoni pa Mungu. Neno linasema “…Mungu huwapinga wajikwezao, bali huwapa neema wanyenyekevu” (Yak 4:6).

Wazazi katika familia, wakinyenyekeana wao kwa wao hapo wanakuza zaidi upendo wao. Kiburi, maringo, dharau na majivuno, hufukuza upendo. Lakini unyenyekevu hukuza na kudumisha upendo. Inapotokea kwa sababu zozote wazazi wanaoneshana umwamba, hakuna anayetaka kujishusha hata pale linapotokea kosa au kwazo la wazi, hapo upendo na furaha ya maisha ya ndoa huingia katika dosari kubwa.

Ndoa nyingi zimeingia katika migogoro ya kudumu sio kwa sababu ya matatizo makubwa, hasha! Pengine ni makosa madogomadogo ya kawaida kabisa ya kibinadamu. Lakini kwa vile hakuna ile hali ya unyenyekevu, kuwa tayari kujishusha, kila mtu anataka kujionesha yeye ni zaidi, na yupo sahihi zaidi ya mwenzake; hapo ndipo mgogoro hukuzwa zaidi.

Hapa rai ya moja kwa moja tunaipeleka kwa wanandoa! Wanandoa tukitaka amani, utulivu na maelewano ndani ya ndoa zetu, tuwe wanyenyekevu. Tukomeshe vilema vya kiburi, dharau, kujiona na maringo. Unyenyekevu ni daraja ya kufikiana na kuafikiana. Ukiwa mnyenyekevu, hata pale unapopatwa na tatizo, mwenzi wako ni rahisi kukuelewa, kukupokea na kukuinua. Lakini ukikosa unyenyekevu, utamfanya mwenzio ashangilie ukipatwa na mabaya.

Unyenyekevu, ni kiti cha kutuweka katika mazungumzo yenye mwafaka daima. Bila unyenyekevu, kila neno utakalotamka litakuwa na virusi vya fujo. Wazazi tukiwa wanyenyekevu, watoto wetu wataiga mwenendo wetu wa unyenyekevu nao pia tutawafundisha unyenyekevu. Sisi wazazi ndio waalimu wa maadili katika Kanisa la nyumbani, basi, na tujitahidi kuwa wanyenyekevu.

Na mtume Paulo anaelekeza kuuambata unyenyekevu, kwani ndiyo njia ya kujenga usitawi. Anasema “msifanye chochote kwa moyo wa fitina au majivuno ya bure; muwe na unyenyekevu ninyi kwa ninyi, na kila mmoja amwone mwenzake kuwa bora kuliko yeye mwenyewe. Pasiwe na mtu anayetafuta faida yake mwenyewe tu, bali faida ya mwenzake” (Fil. 2:3-4).
MWISHO
Bwana, anatualika sisi sote tuwe wanyenyekevu akisema ”jifunzeni kutoka kwangu kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo, nanyi mtapata raha nafsini mwenu”. (Mt. 11:29). Na pengine anatuasa akisema “Anayejikweza atashushwa, na yeyote anayejushusha atakwezwa (Mt 23:12). Unyenyekevu ni ngazi ya kupanda juu, zaidi na zaidi.
“Mtiini Mungu mpingeni shetani naye ata wakimbia”
AMEN.
imeandaliwa na
mwinjilist John
#0768386606